• HABARI MPYA

    Thursday, February 18, 2021

    YANGA SC WASAWAZISHA MARA TATU MFULULIZO KUPATA SARE YA 3-3 NA KAGERA SUGAR LIGI KUU DAR

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    VINARA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga SC jana walilazimika kusawazisha mara tatu mfululizo kupata sare ya kufungana mabao 3-3 na Kagera Sugar Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
    Sare hiyo inayofuatia sare za 1-1 ugenini dhidi ya Tanzania Prisons Sumbawanga mkoani Rukwa na Mbeya City mjini Mbeya inaifanya Yanga SC ifikishe pointi 46 baada ya kucheza mechi 20 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi saba zaidi ya mabingwa watetezi, Simba SC ambao hata hivyo wana mechi tatu mkononi.
    Mabao ya Kagera Sugar iliyokuwa ikitangulia jana yalifungwa na Peter Mwalyanzi dakika ya 11, Hassan Mwaterema dakika ya 24 na Yusuph Mhilu dakika ya 45 akiiadhibu timu yake ya zamani.
    Mabao ya Yanga nayo yalifungwa na Tuisila Kisinda dakika ya 14 kwa penalti baada ya beki wa Kagera Sugar, Abdallah Mfuko kuunawa mpira kwenye boksi na Deus Kaseke dakika ya 30 na Tonombe Mukoko dakika ya 61. 
    Mechi nyingine za Ligi Kuu jana, Mtibwa Sugar ililazimishwa sare ya 1-1 na Ihefu SC Uwanja wa CCM Gairo mkoani Morogoro. Issa Ngoah alianza kuifungia Ihefu dakika ya 13 kabla ya Sabato Kasika kuisawazishia Mtibwa dakika ya 38. Nayo Dodoma Jiji FC ikaichapa Coastal Union 2-1 Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma. Mabao ya Dodoma Jiji yalifungwa na Anuary Jabir dakika ya 57 na Jamal Mtegeta dakika ya 57, wakati l Coastal Union lilifungwa na Raizin Hafidh kwa penalti dakika ya 83. 
    Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Metacha Mnata, Kibwana Shomari, Yassin Mustapha, Lamine Moro, Bakari Mwamnyeto, Zawadi Mauya/Tonombe Mukoko dk46, Tuisila Kisinda, Feisal Salum, Michael Sarpong/Ditram Nchimbi dk46, Deus Kaseke/ Haruna Niyonzima dk74 na Farid Mussa. 
    Kagera Sugar: Said Kipao, Mwaita Gereza, David Luhende, Hassan Isihaka/Yussuf Mlipili dk70, Abdallah Mfuko, Abdulswamad Kassim, Yusuph Mhilu, Abdallah Seseme/Ally Nassor dk74, Hassan Mwaterema/Mohamed Ibrahim dk82, Nassor Kapama na Peter Mwalyanzi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC WASAWAZISHA MARA TATU MFULULIZO KUPATA SARE YA 3-3 NA KAGERA SUGAR LIGI KUU DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top