• HABARI MPYA

    Thursday, February 11, 2021

    AZAM FC YAZIDI KUJIONDOA KWENYE MBIO ZA UBINGWA LIGI KUU, YACHARAZWA 2-1 NA COASTAL UNION MKWAKWANI



    TIMU ya Azam FC imezidi kujiondoa kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuchapwa 2-1 na wenyeji, Coastal Union jioni ya leo Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga.
    Mabao ya Coastal Union yamefungwa na Hijja Ugando dakika ya tisa kwa penalti na Hamad Majimengi dakika ya 54, wakati la Azam FC limefungwa na beki Mghana, Daniel Amoah dakika ya 36.
    Matokeo hayo yanaifanya Coastal Union ifikishe pointi 23 baada ya kucheza mechi 19 na kusogea nafasi ya tisa, ikizidiwa pointi mbili na KMC inayoshika nafasi ya sita.
    Azam FC inayofundishwa na kocha Mzambia, George Lwandamina inabaki na pointi zake 33 baada ya kucheza mechi 19, nyuma ya mabingwa watetezi, Simba SC wenye pointi 39 za mechi 17 na Yanga SC wenye pointi 44 za mechi 18.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Kagera Sugar imelazimishwa sare ya 1-1 na Gwambina FC ya Misungwi mkoani Mwanza Uwanja wa Kaitaba, Bukoba.
    Winga Yussuf Mhilu alianza kuifungia Kagera Sugar dakika ya sita kabla ya Meshack Abraham kuisawazishia Gwambina dakika ya 90 na ushei.
    Kagera Sugar inafikisha pointi 23 baada ya kucheza mechi 19 na ikasogea nafasi ya nane, wakati Gwambina inafikisha pointi 20 baada ya kucheza mechi 18 na inabaki nafasi ya 15.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAZIDI KUJIONDOA KWENYE MBIO ZA UBINGWA LIGI KUU, YACHARAZWA 2-1 NA COASTAL UNION MKWAKWANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top