• HABARI MPYA

    Thursday, March 29, 2018

    MKUTANO MKUU YANGA KUFANYIKA MEI 5 DAR ES SALAAM KUJADILI MUSTAKABALI MPYA WA KLABU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KLABU ya Yanga inatarajiwa kufanya Mkutano wake Mkuu wa mwaka Mei 5 mwaka huu katika ukumbi utakaotajwa baadaye mjini Dar es Salaam.
    Mkutano huo ni matokeo ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya Yanga kilichofanyika Jumapili iliyopita mjini Dar es Salaam chini ya Kaimu Mwenyekiti, Clement Sanga ambacho kimewataka wanachama kujindaa kwa ajenda zitakazotangazwa baadaye.
    Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Yanga SC, Charles Boniface Mkwasa alipozungumza na Waandishi wa Habari makao makuu ya klabu, Jangwani mjini Dar es Salaam.
    Mkwasa, mchezaji na kocha wa zamani wa Yanga pamoja na timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars amesema kwamba mkutano huo utakuwa maalum kwa wanachama kujadili masuala mbalimbali na kwa ujumla mustakabali wa klabu.
    Katibu Mkuu wa Yanga SC, Charles Boniface Mkwasa (kushoto) akizungumza na Waandishi wa Habari makao makuu ya klabu leo. Kulia ni Ofisa Habari, Dissmas Ten 

    Mkwasa amesema kwamba wanachama wa Yanga wanapaswa kufanya maandalizi ya kuhudhuria mkutano huo sasa kwa kulipa ada za uanachama wao mapema, kwa sababu kwenye mkutano huo ukaguzi mkubwa utafanyika kabla ya watu kuingia ndani ya ukumbi.
    “Mkutano utafanyika Mei 5 hapa Jijini Dar es Salaam, wanachama wenye kadi aina zote mbili wataruhusiwa kuingia ukumbuni, kwa maana ya wale wenye kadi za zamani na hizi zinazotolewa sasa kupitia benki ya posta,”amesema Mkwasa, aliyeongozana na Msemaji wa klabu, Dissmas Ten.
    Ikumbukwe Yanga imekuwa chini ya Kaimu Mwenyekiti, Sanga kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Mwenyekiti, Yussuf Manji Mei mwaka jana.
    Manji aliingia Yanga mwaka 2006 kama mdhamini kupitia kampuni yake ya Lotto Kitita, lakini baadaye akawa mfadhili Mkuu wa klabu kabla ya kuwa Mwenyekiti.
    Katika kipindi chake cha kuwa mfadhili na Mwenyekiti wa Yanga, Manji aliifanyia mengi klabu– kubwa ni kuirejeshea hadhi na heshima klabu hiyo.
    Alipoingia mwaka 2006 aliikuta klabu ipo dhoofu kiuchumi na haiwezi kushindana na mahasimu wao, Simba katika kuwania wachezaji bora ambao ndiyo mtaji wa kushinda mataji.
    Wakati huo Yanga ilikuwa inasajili wachezaji ambao ama walikuwa wameachwa na timu zao, waliojipeleka wenyewe kwa mapenzi yao au waliopatikana kwa njia ya mchujo wa majaribio.
    Lakini mara baada ya Manji kuingia Yanga, klabu hiyo ikaanza kusifika kwa kusajili wachezaji wa kigeni na wale nyota wa hapa nyumbani, ikiwa ni pamoja na kubomoa ngome ya mahasimu, Simba SC.
    Mwaka 2009 fedha za Manji zilimtoa kipa kipenzi cha wana Simba Msimbazi, Juma Kaseja na desturi hiyo ikaendelea baadaye wakichukuliwa beki Kelvin Yondan na mshambuliaji Mganda Emmanuel Okwi.
    Yanga iliipiku Simba ‘kimafia’ katika kumsajili beki anayeweza kucheza kama kiungo pia, Mbuyu Twite kutoka APR ya Rwanda, tu kwa jeuri ya fedha.
    Aliyekuwa Mwenyekiti wa Simba, Alhaj Ismail Aden Rage alianza kuonekana akimsainisha Mbuyu mjini Kigali, lakini baadaye Mwenyekiti wa Usajili wa timu ya Jangwani, Abdallah Bin Kleb akaingia kwa ‘gia kubwa’ na kubadilisha mambo, Mbuyu akatua Jangwani.
    Na ni katika kipindi hicho imeshuhudiwa Manji amewazima kabisa Simba na Yanga ikitawala soka ya Tanzania na kuzidi kujiongezea mashabiki na wapenzi.
    Lakini migogoro haikukosekana pia wakati wa utawala wa Manji, ambayo wakati fulani iliiathiri timu mfano ule wa kutaka kumng’oa aliyekuwa Mwenyekiti, Wakili Lloyd Nchunga ulioiponza klabu ifungwe 5-0 na mahasimu, Simba Mei 6, mwaka 2012.
    Mapema mwaka jana, Manji alikuja na mpango wa kutaka kujikodisha klabu kupitia kampuni aliyoisajili kwa jina la Yanga Yetu, lakini ukapata upinzani mkali na kuamua kuachana nao.  
    Kabla ya kufikia maamuzi haya, Manji alipitia kwenye misukosuko na Serikali kuanzia Januari hadi Aprili, kwanza akikamatwa na kuwekwa ndani kwa tuhuma za kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya na baadaye akidaiwa kumiliki pasipoti mbili.
    Hali hiyo ilisababisha ashindwe kutekeleza majukumu yake ya kiufadhili Yanga na kufanya wachezaji wakose mishahara kwa kipindi chote hicho kabla ya viongozi wenzake kuanza kufanya jitihada za kulipa taratibu.
    Lakini kwa ujumla ni udhamini wa SportPesa ndiyo umekuwa mkombozi wa tatizo la kiuchumi la Yanga baada ya Manji kuondoka, ingawa hali ya kifedha bado si nzuri klabu na hilo linatarajiwa kuwa miongoni mwa mambo yatakayajadiliwa Mei 5.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MKUTANO MKUU YANGA KUFANYIKA MEI 5 DAR ES SALAAM KUJADILI MUSTAKABALI MPYA WA KLABU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top