• HABARI MPYA

    Saturday, March 31, 2018

    MTIBWA SUGAR WAENDA NUSU FAINALI AZAM SPORTS FEDERATION CUP KWA MATUTA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Mtibwa Sugar imefanikiwa kwenda Nusu Fainali ya michuano ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) baada ya ushindi wa penalti 9-8 kufuatia sare ya 0-0 ndani ya dakika 90.
    Maana yake sasa, Azam FC wanaweza kuikosa michuano ya Afrika kwa mara ya pili mwakani, kwani mwenendo wao kwenye Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara tayari si wa mwelekeo wa ubingwa, wakiwa wanaachwa na vigogo Simba na Yanga kwa pointi mbili na wana mechi mbili zaidi pia za kucheza. 
    Baada ya dakika 90 ngumu timu hizo zikimaliza bila kufungana, kila timu ikaenda kupiga mikwaju 10 ya penalti, Mtibwa Sugar wakikosa moja na wakikosa mbili.
    Kipa wa Mtibwa, Marcos Tinocco alipangua penalti ya mwisho ya beki Abdallah Kheri baada ya Frank Domayo kugongesha mwamba  mkwaju wake wa tatu, wakati Mwadini Ali wa Azam FC alipangua shuti la mkongwe, Henry Joseph Shindika. 
    Waliofunga penalti za Azam FC ni Nahodha Himid Mao, Yahya Zayed, Mzimbabwe Bruce Kangwa, Aggrey Morris, Joseph Kimwaga, Joseph Mahundi, Swaleh Abdallah na Salum Abubakar ‘Sure Boy’.
    Waliofunga penalti za Mtibwa Sugar ni Hassan Dilunga, Ismail Muhesa, Stahmil Mbonde, Shaaban Nditi, Hassan Isihaka, Hassan Mganga, Salim Kihimbwa, Cassian Ponera na Dickson Daudi.
    Mtibwa sasa itamenyana na Stand United katika Nusu Fainali, ambayo jana iliitoa Njombe Mji FC kwa kuichapa 1-0 Uwanja wa CCM Kambarage, Shinyanga.
    JKT Tanzania imekuwa timu nyingine kuingia Nusu Fainali leo kwa kuwafunga wenyeji, Tanzania Prisons 2-0 Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya na yenyewe itakutana na mshindi wa Robo Fainali ya mwisho kesho kati ya wenyeji, Singida United na Yanga Uwanja wa Namfua. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR WAENDA NUSU FAINALI AZAM SPORTS FEDERATION CUP KWA MATUTA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top