• HABARI MPYA

    Tuesday, October 06, 2015

    YANGA SC ‘YAMTEMA’ MKWASA AELEKEZE NGUVU TAIFA STARS

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    YANGA SC imesema kwamba Charles Boniface Mkwasa anamaliza Mkataba wake Desemba na hawana tatizo naye iwapo hataongeza Mkataba.
    Katibu wa Yanga SC, Dk. Jonas Tiboroha amesema kwamba wanasikia tu juu ya mpango wa Mkwasa kusaini Mkataba wa kuwa kocha wa kudumu wa timu ya taifa, Taifa Stars na hawana pingamizi.
    Leo Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amesema kwamba Mkwasa atasaini Mkataba wa kudumu Taifa Stars, sawa na wa mtangulizi wake, Mholanzi Mart Nooij.   
    Malinzi alimteua Mkwasa kukaimu Ukocha Mkuu Taifa Stars kwa miezi mitatu tangu Julai na akasema kwa kuanzia atakuwa anachukua mshahara alikuwa analipwa Nooij. 
    Charles Boniface Mkwasa sasa atakuwa kocha wa Taifa Stars pekee 

    Nooij aliyekuwa analipwa dola za Kimarekani 12,500 (zaidi ya Sh. Milioni 25) kwa mwezi, alifukuzwa mwishoni mwa Juni baada ya Taifa Stars kufungwa mabao 3-0 na Uganda Uwanja wa Amaan, Zanzibar katika mechi ya kufuzu CHAN.
    Mkwasa aliwateua Alhaj Abdallah Athumani Seif ‘King Kibaden’ kuwa Mshauri wa Ufundi, Hemed Morocco kuwa Kocha Msaidizi na Manyika Peter kuwa kocha wa makipa wakichukua nafasi za Salum Mayanga na Patrick Mwangata.
    Aidha, Omar Kapilima aliteuliwa kuwa Meneja na Hussein Swedi ‘Gaga’ kuwa mtunza vifaa vya timu- kukamilisha sura mpya kabisa ya benchi la Ufundi la Taifa Stars.
    Na tangu hapo timu imcheza mechi tatu bila ushindi ikitoa sare ya 1-1 na Uganda mjini Kampala kufuzu CHAN, ikifungwa 2-1 na Libya mchezo wa kirafiki mjini Kartepe, Uturuki na kutoa sare ya 0-0 na Nigeria Septemba 5 Dar es Salaam.
    Hayo yalikuwa mabadiliko makubwa kutoka kwenye timu kufungwa mechi tano mfululizo na kwa ujumla kucheza mechi 11 bila ushindi chini ya Nooij.
    Mkwasa anatarajiwa kuiongoza Taifa Stars katika mchezo wa nne kesho, itakapomenyana na Malawi kuwania kufuzu Kombe la Dunia. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC ‘YAMTEMA’ MKWASA AELEKEZE NGUVU TAIFA STARS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top