• HABARI MPYA

    Tuesday, July 01, 2014

    HANS POPPE: F.O.S. NI UKUTA WA CHUMA, SIMBA SC SASA WAPINZANI WATAISIKIA KWENYE BOMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MWENYEKITI wa Friends Of Simba (F.O.S.), Zacharia Hans Poppe amesema umoja wao ni sawa na ukuta wa chuma, maana yake wapinzani wa Simba SC katika soka ya Tanzania sasa wasitarajie mteremko kwa klabu hiyo.
    Kwa miaka mitatu sasa Simba SC haijatwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na pia haijashiriki michuano ya Afrika.
    Lakini baada ya kigogo wa F.O.S., Evans Elieza Aveva kuchaguliwa kuwa Rais wa kwanza wa klabu hiyo Jumapili, Simba SC inatarajiwa kurejesha makali yake.
    Mwenyekiti wa F.O.S., Zacharia Hans Poppe amesema Simba SC sasa itacheza mpira

    Kapteni wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Poppe amesema kwamba Friends Of Simba ni ukuta wa chuma.
    “Lango la Simba SC sasa liko salama, Friends Of Simba ni beki imara, haipitiki, sawa na ukuta wa chuma, sasa tunakwenda kucheza mpira, nawaomba wana Simba SC wote waliojitenga kwa sababu ya matokeo mabaya, warudi uwanjani timu yao ikicheza, watafurahi,”amesema.
    Poppe amesema uongozi uliopita wa Alhaj Ismail Aden Rage haukuwa na ushirikiano, uliwagawa wanachama na akiwa Mjumbe wa Kamati ya Utendaji alijitahidi kumshauri Mwenyekiti wake, lakini hakusikilizwa.
    “Nilitumia muda wangu mwingi kumshauri Rage, lakini hakunisikiliza. Friends tulikuwa tunachangishana fedha, nampelekea Rage akafanyie shughuli za klabu. Baadaye yeye anakwenda kusema, ni fedha za klabu.
    Wewe unadhani waliotoa fedha zao watajisikiaje? Basi, Friends wakaanza kujitenga na huo ndiyo ukawa mwanzo wa Simba SC kufanya vibaya, sababu hamasa ilipotea na wachezaji wakatumbukiwa nyongo.
    Mishahara ikawa inachelewa, mfumo mzima wa malipo ya wachezaji ukawa haueleweki, timu ikawa ipo ipo tu. Lakini sasa tuna uongozi ambao utasikiliza ushauri na kuufanyia kazi. Uongozi ambao utaifanya Simba  SC kuwa ya wana Simba wote,”amesema Hans Poppe.
    Poppe amesema anafahamu kuna ushindani mkali hivi sasa katika Ligi Kuu kutoka kwa mabingwa, Azam FC, wapinzani wao wa jadi, Yanga SC walioshika nafasi ya pili na hata Mbeya City, waliomaliza nafasi ya tatu, lakini wao (F.O.S.) watatumia uwezo na uzoefu wao kuicheza Ligi wamalize juu ya timu zote hizo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HANS POPPE: F.O.S. NI UKUTA WA CHUMA, SIMBA SC SASA WAPINZANI WATAISIKIA KWENYE BOMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top