• HABARI MPYA

    Saturday, December 10, 2022

    MESSI AIVUSHA ARGENTINA, BRAZIL YA NEYMAR NJE KOMBE LA DUNIA


    TIMU ya Taifa ya Argentina imefanikiwa kutinga Nusu Fainali ya Kombe la Dunia huku wapinzani wao wa Amerika Kusini, Brazil wakitolewa katika mechi mbili tamu za jana zilizoamuliwa kwa mikwaju ya penalti.
    Ilianza Croatia kuitoa Brazil kwa penalti 4-2 baada ya sare ya 1-1, kabla ya Argentina kuitupa nje Uholanzi kwa penalti 4-3 kufuatia sare ya 2-2 ndani ya dakika 120.
    Katika mechi ya kwanza, Brazil ilitangulia kwa bao la Neymar dakika ya 105, kabla ya Bruno Petković kuisawazishia Croatia dakika ya 117 Uwanja wa Education City Jijini Al Rayyan.
    Katika mikwaju ya penalti, waliofunga za Croatia ni N. Vlašić, L. Majer, L. Modrić na M. Oršić, wakati Brazil ni Casemiro na Pedro pekee walifunga huku Rodrygo na Marquinhos wote wakikosa.



    Baadaye Uwanja wa Lusail Iconic mjini Lusail, Argentina ilitangulia kwa mabao ya Nahuel Molina dakika ya 35 na Nahodha Lionel Messi dakika ya 73 kwa penalti, lakini Uholanzi ikasawazisha kupitia kwa Wout François Maria Weghorst dakika ya 83 na 90 na ushei.
    Waliofunga penalti za Argentina ni Messi, Leandro Paredes, G. Montiel na Lautaro Martínez huku Enzo Jeremías Fernández akikosa na kwa kwa upande wa Uholanzi waliofunga ni T. Koopmeiners, Weghorst na L. de Jong huku V. van Dijk na S. Berghuis wakikosa.
    Sasa Argentina itakutana na Croatia katika Nusu Fainali, wakati Robo Fainali za mwisho zinapigwa leo, Morocco na Ureno Saa 12:00 jioni na England dhidi ya Ufaransa Saa 4:00 usiku.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MESSI AIVUSHA ARGENTINA, BRAZIL YA NEYMAR NJE KOMBE LA DUNIA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top