• HABARI MPYA

    Tuesday, January 31, 2017

    SIMBA YAMUACHIA MAUMIVU MKATA UMEME WA AZAM

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BAADA ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, kuanza rasmi mazoezi jana jioni kujiandaa na mchezo ujao dhidi ya Ndanda, daktari wa timu hiyo, Mwanandi Mwankemwa, amezungumzia hali za kiafya za baadhi ya wachezaji waliokuwa majeruhi.
    Wachezaji wa Azam FC waliokuwa majeruhi ni nahodha John Bocco ‘Adebayor’, Stephan Kingue waliopata majeraha ya misuli ya paja kwenye mchezo uliopita wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) dhidi ya Simba, ambao matajiri hao walishinda bao 1-0 lililofungwa na Bocco.
    Stephan Kingue aliumia katika mechi dhidi ya Simba Jumamosi 

    Wengine wanaouguza majeraha, ambao waliukosa mchezo huo ni kiungo Salum Abubakar ‘Sure Boy’, kipa Mwadini Ally (nyama za paja) na beki Shomari Kapombe, ambaye ni mgonjwa lakini hivi sasa akiendelea vema.
    Akizungumza leo baada ya mazoezi, Mwankemwa alisema kuwa Bocco na Kingue watakaa nje ya dimba kwa muda wa wiki mbili tokea jana, huku Sure Boy akitarajiwa kuanza rasmi mazoezi leo na Mwadini akipumzishwa kwa siku tatu kuanzia jana.
    “Bocco hali yake inaonekana kuimarika vizuri tokea alipopata majeraha hayo ya kuchana msuli wa nyuma ya paja, Stephan (Kingue) kwa upande wake naye amechana msuli wa mbele ya paja, hivyo wote watakaa nje ya dimba kwa muda wa wiki mbili kutoka sasa (jana) na wataanza mazoezi mepesi baada ya wiki moja,” alisema.
    Daktari huyo bingwa mzoefu, alisema hali za wachezaji wengine ziko vizuri kabisa kuendelea na mikikimikiki ya maandalizi kuelekea mechi zijazo za ligi pamoja na michuano mingine.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YAMUACHIA MAUMIVU MKATA UMEME WA AZAM Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top