• HABARI MPYA

    Monday, March 06, 2017

    YANGA YALIMWA FAINI KWA KUPITIA 'MLANGO WA UANI' DHIDI YA SIMBA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    YANGA SC imetozwa faini ya Sh. 500,000 kwa kupitia mlango usio rasmi kuingia Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya mahasimu, Simba SC Februari 25, mwaka huu.
    Adhabu hiyo imetolewa na Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi Tanzania (Kamati ya Saa 72), katika kikao chake cha Machi 4, mwaka huu kuptia matukio mbalimbali ya Ligi Kuu msimu wa 2016/2017 unaoendelea sasa.
    Katika mechi hiyo namba 169, Yanga ilifungwa mabao 2-1 licha ya kuongoza kwa 1-0 hadi mapumziko kutokana na bao la penalti la Simon Msuva, lakini kipindi cha pili Simba ikazinduka kwa mabao ya Laudit Mavugo na Shiza Kichuya.
    Taarifa ya Kamati leo imesema kwamba kitendo hicho ni kwenda kinyume cha kanuni ya 14 (14) ya Ligi Kuu inayoelekeza kuwa timu zitaingia uwanjani kwa kutumia milango rasmi.
    Rais wa TFF, Jamal Malinzi akiwakagua wachezaji wa Yanga kabla ya mechi na Simba Februari 25

    Kikao hicho pia kilifuta kadi nyekundu ya mshambuliaji Obrey Chirwa wa Yanga aliyoonyeshwa katika mchezo dhidi ya Ruvu Shooting Uwanja wa Taifa, Machi 1 kwa kumuondolea kadi ya kwanza ya kwanza ya njano aliyoonyeshewa siku hiyo.
    Kadi hiyo imefutwa kwa mujibu wa kanuni ya 9 (8) baada ya Kamati ya Saa 72 haikupaswa kutolewa kwa Chirwa kwa sababu hakukuwa na kosa wala mazingira ya kuonywa.
    Kadi hiyo ilikuwa ni msingi wa kadi nyekundu baada ya Chirwa kufanya faulo ambayo aliadhibiwa tena kwa kadi ya njano hivyo kutolewa nje kwa mujibu wa taratibu.
    Kufutwa kwa kadi ya njano ya kwanza, kunapelekea kufutwa kwa kadi nyekundu ambayo msingi wa kadi hiyo ulisababisha kadi nyekundu hivyo mchezaji angempaswa kukosa mchezo mmoja. Hata hivyo, kadi ya pili ya njano inahesabiwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA YALIMWA FAINI KWA KUPITIA 'MLANGO WA UANI' DHIDI YA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top