• HABARI MPYA

    Friday, December 24, 2021

    KIBU APIGA MBILI SIMBA SC YAITANDIKA KMC 4-1 TABORA


    MABINGWA watetezi, Simba SC wametoa onyo kali baada ya kuitandika KMC mabao 4-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Ally Hassan Mwinyi mjini Tabora.
    Mabao ya Simba SC yamefungwa na mabeki, Mohamed Hussein ‘ Tshabalala’, dakika ya 10, Mkenya Joash Onyango dakika ya 12 na mshambuliaji Kibu Dennis mawili dakika ya 46 na 56, wakati la KMC limefungwa na Abdul Hillary dakika ya 41.
    Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi 21, ingawa inabaki nafasi ya pili ikizidiwa pointi mbili na vinara, Yanga SC baada ya timu zote kucheza mechi tisa.
    KMC yenyewe inabaki na pointi zake 10 katika nafasi ya 11 baada ya kucheza mechi 10 sasa.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, wenyeji, Coastal Union wameibuka na ushindi wa 3-2 dhidi ya Mbeya City Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga.
    Mabao ya Coastal Union yamefungwa na Abdul Suleiman ‘Sopu’ dakika ya 10 na la penalti dakika ya 90 na lingine Hajji Ugando dakika ya 45 na ushei, wakati ya Mbeya City yamefungwa na Juma Luizio dakika ya 33 na Richardson Ng’ondya kwa penalti dakika ya 72.
    Coastal Union inafikisha pointi 17 na kupanda nafasi ya tatu ikiizidi pointi mbili Mbeya City inayoshukia nafasi ya sita baada ya timu zote kucheza mechi 10 sasa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KIBU APIGA MBILI SIMBA SC YAITANDIKA KMC 4-1 TABORA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top