• HABARI MPYA

    Sunday, December 26, 2021

    YANGA YATOKA NYUMA TENA KUILAZA BIASHARA 2-1


    WENYEJI, Yanga SC wametoka nyuma na kushinda 2-1 dhidi ya Biashara United katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara usiku huu Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Biashara walitangulia kwa bao la Atupele Green Jackson dakika ya pili tu, kabla ya mshambuliaji Fiston Kalala Mayele kuisawazishia Yanga SC dakika ya 40 kwa bao zuri la til-tak akimalizia krosi ya Mkongo mwenzake, beki Djuma Shabani kutoka upande wa kulia.
    Kiungo mkongwe Mrundi, Said Ntibanzokiza akaifungia bao la ushindi Yanga dakika ya 79 kwa penalti baada ya beki Abdulmajid Mangaro kumsukuma winga Mkongo, Jeses Moloko Ducapel upande ule ule wa kulia.
    Yanga inafikisha pointi 26 katika mchezo wa 10 na kuendelea kuongoza ligi kwa pointi tano zaidi ya mabingwa watetezi, Simba SC ambao hata hivyo wana mechi moja mkononi.
    Biashara United yenyewe baada ya kipigo cha leo ambacho ni cha tatu mfululizo ikitoka kufungwa 2-0 na Mtibwa Sugar Morogoro na 1-0 na Coastal Union nyumbani, Musoma inabaki na pointi zake nane za mechi 11 sasa katika nafasi ya 15 kwenye ligi ya timu 16.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA YATOKA NYUMA TENA KUILAZA BIASHARA 2-1 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top