• HABARI MPYA

    Thursday, July 15, 2021

    FEISAL SALUM ‘FEI TOTO’ APIGA ZOTE MBILI YANGA SC YAICHAPA IHEFU SC 2-0 NA KUNG’ANGA’NIA NYUMA YA MABINGWA, SIMBA SC

    MABAO ya kiungo Feisal Salum Abdallah ‘Fei Toto’ dakika ya 17 na 37 yametosha kuwapa Yanga SC ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Ihefu SC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Yanga SC imefikisha pointi 73 baada ya ushindi huo katika mchezo wa 33, ingawa inabaki nafasi ya pili nyuma ya mabingwa tayari kwa mara ya nne mfululizo, Simba SC wenye pointi 79 za mechi 32.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, Coastal Union ya Tanga imeibuka na ushindi wa 5-0 dhidi ya Mwadui FC Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga, mabao ya Rashid Chambo dakika ya nane, Issa Abushehe dakika ya 17, Raizin Hafidh dakika ya 66 na Mudhathir Abdallah dakika ya 82 na 90.
    Nao Kagera Sugar wakaibuka na ushindi wa ugenini wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Polisi Tanzania bao pekee la Hassan Mwaterema dakika ya 46 Uwanja wa Ushirika mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.
    Na Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya, wenyeji Mbeya City wakaibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Gwambina bao pekee la Kibu Denis dakika ya 73, wakati Dodoma Jiji FC imelazimishwa sare ya 0-0 na Mtibwa Sugar Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma.
    Mechi za mchana KMC imeshinda 5-2 dhidi ya JKT Tanzania Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam, Sadallah Lipangile akifunga mabao mawili dakika za 15 na 43 sawa na Charles Ilanfya dakika ya 45 na ushei na 72 na Cliff Buyoya dakika ya 79, huku ya wageni yakifungwa na Daniel Lyanga dakika ya 45 na Bilal dakika ya 63.
    Nayo Ruvu Shooting ikaichapa Namungo FC 2-1 mabao yake yakifungwa na David Richard dakika ya 27 na Fully Maganga dakika ya 63, wakati la wageni limefungwa na Reliants Lusajo dakika ya 79 Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.
    Na Uwanja wa Mandela, Sumbawanga mkoani Rukwa bao la Mohammed Mkopi dakika ya 56 liliwasaidia wenyeji, Tanzania Prisons kupata sare ya 1-1 na Biashara United ya Mara iliyotangulia kwa bao la Christian Zigah dakika ya 47.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: FEISAL SALUM ‘FEI TOTO’ APIGA ZOTE MBILI YANGA SC YAICHAPA IHEFU SC 2-0 NA KUNG’ANGA’NIA NYUMA YA MABINGWA, SIMBA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top