• HABARI MPYA

    Wednesday, May 01, 2019

    AMUNIKE AMREJESHA AJIBU KIKOSINI TAIFA STARS, AMUITA NA ADI ANAYECHEZA ENGLAND

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Emmanuel Amunike ametaja kikosi cha awali cha wachezaji 39 kwa ajili ya mchezo wa kirafiki na Misri Juni 13, mwaka huu Uwanja wa Borg El Arab mjini Alexandria kujiandaa na Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
    Amunike ametaja kikosi hicho leo na akasema pia kitahusu pia mchezo wa kufuzu Fainali za Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN) zinazohusu wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee dhidi ya Sudan mwishoni mwa Julai.
    Kikosi hicho kinaundwa na makipa; Aishi Manula (Simba SC), Metacha Mnata (Mbao FC), Suleiman Salula (Malindi SC) na Aaron Lulambo (Tanzania Prisons).

    Ibrahim Ajibu (kulia) ameitwa kwenye kikosi cha awali cha wachezaji 39 kwa ajili ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Misri Juni 13, mwaka huu mjini Alexandria 

    Mabeki; Claryo Boniface (U20), Hassan Kessu (Nkana FC, Zambia), Vincent Philipo (Mbao FC), Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Erasto Nyoni (Simba SC), Kelvin Yondan, Gardiel Michael (Yanga SC), Abdi Banda (Baroka FC, Afrika Kusini), Ally Mtoni (Lipuli FC), David Mwantika, Aggrey Morris (Azam FC), Ally Ally (KMC) na Kennedy Wilson (Singida United).
    Viungo ni Feisal Salum, Ibrahim Ajibu (Yanga SC), Himid Mao (Petrojet, Misri), Frank Domayo, Mudathir Yahya (Azam FC), Jonas Mkude (Simba SC), Shiza Kichuya (ENNPI, Misri), Simon Msuva (Difaa Hassan El-Jadidi Morocco), Farid Mussa (Tenerife, Hispania) na Freddy Tangalu (Lipuli FC).
    Washambuliaji ni Yahya Zayd (Ismailia, Misri), Shaaban Iddi Chilunda (Tenerife, Hispania), Rashid Mandawa (BDF, Botswana), Ayoub Lyanga (Coastal Union), Kassim Khamis (Kagera Sugar), Miraj Athumani (Lipuli FC), Kelvin John (Serengeti Boys), Adi Yussuf (Solihull Moors, England), John Bocco (Simba SC), Thomas Ulimwengu (JS Saoura, ALgeria) na Nahodha Mbwana Samatta (KRC Genk, Ubelgiji).  
    Taifa Stars imepangwa Kundi C AFCON 2019 pamoja na jirani zao, Kenya, Algeria na Senegal, wakati Misri ambao ni wenyeji wapo Kundi A pamoja na na Zimbabwe, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Kundi B linaundwa na Burundi, Madagascar, Guinea na Nigeria, Kundi D linaundwa na Namibia, Afrika Kusini, Ivory Coast na Morocco, wakati Kundi E kuna Angola, Mauritania, Mali na Tunisia na Kundi F ni Guinea Bessau, Benin, Ghana na mabingwa watetezi, Cameroon. 
    Taifa Stars imefuzu AFCON ya mwaka huu baada ya kumaliza nafasi ya pili kwenye Kundi L kwa pointi zake nane, nyuma ya jirani zao wa Afrika Mashariki, Uganda walioongoza kwa pointi zao 13 wakizipiku Lesotho iliyomaliza na pointi sita na Cape Verde pointi tano.    
    Mwaka huu, Tanzania itashiriki AFCON kwa mara ya pili tu kihistoria baada ya mwaka 1980 nchini Nigeria ambako ilipangwa Kundi A pamoja na wenyeji, Nigeria, Misri na Ivory Coast na kushika mkia.
    Mwaka 1980 ilifungwa mechi mbili, 3-1 na Nigeria na 2-1 na Misri kabla ya kutoa sare ya 1-1 na Ivory Coast na kuishia Raundi ya kwanza tu, wakati timu nane tu zinashiriki michuano hiyo.   
    Michuano itaanza Juni 21 hadi Julai 19 na Taifa Stars itachezea mechi zake Uwanja wa Juni 30 na Al Salam mjini Cairo.
    Na katika CHAN, Taifa Stars itaanzia nyumbani dhidi ya Sudan Julai 26 kabla ya kurudiana Agosti 2 na ikifuzu mtihani huo itamenyana na mshindi kati ya Kenya na Burundi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AMUNIKE AMREJESHA AJIBU KIKOSINI TAIFA STARS, AMUITA NA ADI ANAYECHEZA ENGLAND Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top