• HABARI MPYA

    Wednesday, May 08, 2019

    SIMBA SC YAITANDIKA COASTAL UNION 8-1 UHURU, OKWI NA KAGERE WAPIGA HAT TRICK

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imepanda kileleni mwa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya ushindi wa kibabe wa mabao 8-1 dhidi ya Coastal Union jioni ya leo Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    Kwa ushindi huo mnono, Simba SC siyo tu imeendeleza ubabe katika Ligi Kuu, bali pia imekamata usukani ikifikisha pointi 81 baada ya kucheza mechi 31, sasa ikiwazidi pointi moja watani wao wa jadi, Yanga SC ambao hata hivyo wamecheza mechi tatu zaidi. 
    Washambuliaji wa kigeni, Meddie Kagere na Emmanuel Okwi kila mmoja amefunga mabao matatu kwenye ushindi huo, huku mabao mengine yakifungwa na viungo Hassan Dilunga na Clatous Chama wakati bao pekee la Coastal limefungwa na Raizin Hafidh.


    Okwi mshambuliaji wa kimataifa wa Uganda alifunga mabao yake dakika za 11, 20 na 47, wakati mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Kagere mzaliwa wa Uganda alifunga mabao yake dakika za 69,65 ma 83.
    Kiungo mzawa, Hassan Dilunga alifunga bao la sita dakika ya 81, wakati kiungo wa kimataifa wa Zambia, Clatous Chama alifunga la nane dakika ya 90 na ushie na Raizin aliifungia Coastal la kufutia machozi dakika ya 35.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo zimemalizika kwa sare, Tanzania Prisons ikitoka 0-0 na Ndanda SC Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya na Mtibwa Sugar imefungana 2-2 na  JKT Tanzania Uwanja wa manungu, Turiani mkoani Morogoro.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Aishi Manula, Nicholas Gyan, Yussuf Mlipili, Erasto Nyoni, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Jonas Mkude, Clatous Chama, Said Ndemla/Mohammed ‘Mo’ Ibrahim dk78, Rashid Juma/Hassan Dilunga dk68, Meddie Kagere na Emmanuel Okwi/Adam Salamba dk68.
    Coastal Union: Soud Abdallah, Miraji Adam, Ibrahim Ame/Bakari Mtwiku dk63, Bakari Mwamnyeto, Adeyum Saleh, Said Jeilan, Haji Ugando, Mtenje Juma, Andrew Simchimcha, Ayoub Lyanga na Raizan Hafidh.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YAITANDIKA COASTAL UNION 8-1 UHURU, OKWI NA KAGERE WAPIGA HAT TRICK Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top