• HABARI MPYA

    Thursday, May 23, 2019

    COASTAL UNION, ALLIANCE FC ZATUMIA VYEMA VIWANJA VYA NYUMBANI KUWACHAPA WAPINZANI

    Na Mwandishi Wetu, TANGA
    TIMU ya Coastal Union ya Tanga imeutumia vyema Uwanja wa nyumbani, Mkwakwani mjini Tanga baada ya kuibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Tanzania Prisons jioni ya leo katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
    Ushindi huo umetokana na bao la mmoja wa washambuliaji wake chipukizi na tegemeo, Raizin Hafidh dakika ya 70 kwenye mchezo huo uliokuwa mkali jioni ya leo.
    Kutokana na ushindi huo, Coastal Union inayofundishwa na Juma Mgunda inafikisha pointi 47 baada ya kucheza mechi 37 na kupanda hadi nafasi ya 10 kutoka ya 12, wakati Tanzania Prisons inabaki na pointi zake 43 katika nafasi ya 14 kwenye ligi ya timu 20.  
    Mchezo mwingine wa Ligi Kuu leo, wenyeji Alliance FC wameibuka na ushindi wa 3-2 dhidi ya Stand United Uwanja wa Nyamagana mjini Mwanza.
    Mabao ya Alliance FC yamefungwa na Dickson Ambundi dakika ya pili na ya 19 na Juma Nyangi dakika ya 47, wakati ya Stand United yamefungwa na William Kimanzi dakika ya 44 na Six Mwakasega dakika ya 53. 
    Sasa Alliance FC ni ya tisa kwenye msimamo wa Ligi Kuu baada ya kufikisha pointi 47 kufuatia kucheza mechi 37, wakati Stand United inabaki na pointi zake 44 za mechi 37 pia katika nafasi ya 12.   
    Tayari Simba SC ni mabingwa baada ya kujikusanyia pointi 91, ambazo haziwezi kufikiwa na timu nyingine yoyote, wakati African Lyon imekwishateremka daraja moja kwa moja na itaungana na timu itakayoshika nafasi ya 19.
    Timu nyingine mbili, ya 17 na 18 zitacheza mechi maalum dhidi ya Pamba na Geita Gold za Daraja la Kwanza kuwania kubaki Ligi Kuu, wakati Namungo FC ya Lindi na Polisi ya Kilimanjaro zimepanda kwa moja moja.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: COASTAL UNION, ALLIANCE FC ZATUMIA VYEMA VIWANJA VYA NYUMBANI KUWACHAPA WAPINZANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top