• HABARI MPYA

    Wednesday, July 06, 2022

    AZAM FC YASAJILI BEKI WA RUVU SHOOTING


    KATIKA kuendelea kujiimarisha kuelekea msimu ujao, klabu ya Azam FC imemsajili beki wa kulia, Nathaniel Chilambo kutoka Ruvu Shooting kwa mkataba wa mwaka mmoja.
    Taarifa ya Azam FC imesema kwamba Chilambo amesaini mkataba huo mbele ya mmiliki wa timu, Yusuf Bakhresa na Afisa Mtendaji Mkuu, Abdulkarim Amin ‘Popat’ wenye kipengele cha kuongeza  baada ya miezi sita kutokana na kiwango atakachokionyesha.
    Beki huyo, mwenye umri wa miaka 19, anayetumia miguu yote miwili kwa ufasaha, mwenye uwezo pia wa kucheza beki ya kushoto, amekuwa na kiwango bora kabisa msimu uliopita.
    Usajili huu ni mwendelezo wa sera za Azam FC kukuza vipaji vya wanasoka vijana wadogo na kuheshimu vipaji vya wachezaji wazawa na wanaamini Chilambo atakuja kuwa msaada mkubwa kwenye timu yao.



    Huyo anakuwa mchezaji mpya wa sita kuelekea msimu ujao na watatu mzawa baada ya viungo washambuliaji, Abdul Hamisi Suleiman ‘Sopu’ kutoka Coastal Union na Cleophace Mkandala kutoka Dodoma Jiji.
    Wengine ni viungo washambuliaji, Kipre Junior na Tape Edinho kutoka Ivory Coast na kiungo mkabaji kutoka Nigeria, Isah Ndala - usajili wa safari hii ukifanywa na mmiliki wa timu mwenyewe, Yussuf Bakhresa kwa kushirikiana na Mtendaji Mkuu, Abdukkarim Amin ‘Popat’.
    Azam FC imeimarisha benchi la ufundi kwa kumrejesha aliyewaji kuwa mchezaji na kocha wake Msaidizi, Kali Ongala safari hii akipewa jukumu la kocha wa mazoezi ya utimamu wa mwili, yaani feetness coach.
    Aidha, pia imemuajiri kocha mpya wa makipa, Mspaniola, Dani Cadena ambaye amewahi kufundisha klabu za Sevilla na Real Betis za Hispania na nyingine za China na Asaudi Arabia akiwa na uzoefu mkubwa na elimu ya juu ya Shirikisho la Soka la Ulaya UEFA.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YASAJILI BEKI WA RUVU SHOOTING Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top