• HABARI MPYA

    Tuesday, December 10, 2019

    KILIMANJARO STARS YAICHAPA ZANZIBAR HEROES 1-0 NA KUBISHA HODI NUSU FAINALI CHALLENGE

    Na Mwandishi Wetu, KAMPALA
    TANZANIA Bara imefufua matumain ya kwenda Nusu Fainali ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya Zanzibar leo Uwanja wa Lugogo mjini Kampala, Uganda.
    Pongezi kwa mfungaji wa bao pekee la Kilimanjaro Stars leo, mshambuliaji wa Azam FC, Ditram Nchimbi Duma anayecheza kwa mkopo Polisi Tanzania, zote za Ligi Kuu ya Bara.
    Nchimbi, mchezaji wa zamani wa Njombe Mji FC, Maji Maji ya Songea na Mwadui FC, alifunga bao hilo dakika ya 39 akimalizia mpira uliotemwa na kipa Suleiman Ahmed Ali ‘Selula’ kufuata shuti la mshmabuliaji wa Buildcon ya Zambia, Eliuter Mpepo aliyemalizia pasi ya kiungo wa Simba SC, Jonas Gerald Mkude.


    Kwa ushindi huo wa kwanza, Kilimanjaro Stars inayofundishwa na Juma Mgunda anayesaidiwa na Zubery Katwila baada ya kufungwa 1-0 katika mchezo wa kwanza, itahitaji ushindi katika mechi ya mwisho na Sudan Jumamosi ili kwenda Nusu Fainali.
    Zanzibar inayofundishwa na Hemed Suleiman ‘Morocco’, nayo pia baada ya sare ya 1-1 na Sudan katika mchezo wa kwanza, itahitaji ushindi kwenye mechi ya mwisho na Kenya kuangalia uwezekano wa kwenda Nusu Fainali kwa wastani wa mabao iwapo Bara itatoa sare au kufungwa na Sudan yenye pointi moja.
    Kenya, au Harambee Stars amabo ndiyo mabingwa watetezi wa michuano hiyo, tayari wamekwishasonga Nusu Fainali baada ya leo pia kushinda 2-1 dhidi ya Sudan katika mchezo wa kwanza.  
    Kikosi cha Tanzania Bara kilikuwa; Aishi Manula, Mwaita Gereza, Gardiel Michael, Bakari Mwamnyeto, Kelvin Yondani, Jonas Mkude, Hassan Dilunga/Cleophace Mkandala dk76, Muzamil Yassin, Miraji Athumani ‘Madenge’/ Nickson Kibabage dk88, Ditram Nchimbi na Eliuter Mpepo.
    Zanzibar; Suleiman Ahmed Ali, Jabir Haruna Abdullah/ Makame Khamis Mussa dk46, Mwinyi Haji Mngwali, Abdallah Kheri Salum/Mohamed Othman Mmanga dk73, Ali Hamad Ali, Faisal Abdallah Salum, Mudathiri Yahya Abbas/Maulid Hassan Nassor dk31, Mohammed Issa Juma ‘Banka’, Abdulaziz Makame, Abalkassim Khamis Suleiman na Dau Issa Haidar.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KILIMANJARO STARS YAICHAPA ZANZIBAR HEROES 1-0 NA KUBISHA HODI NUSU FAINALI CHALLENGE Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top