• HABARI MPYA

    Friday, December 23, 2016

    YANGA WAWEKA SHIDA PEMBENI .WAINGIA UWANJANI KWA NGUVU MOJA LEO KUINYOOSHA AFRICAN LYON

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    KOCHA Mzambia wa Yanga, George Lwandamina amesema kwamba wachezaji wamemuahidi kusahau matatizo yao ya mishahara na kuingia kwa nguvu moja katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara leo dhidi ya African Lyon.
    Yanga watakuwa wageni wa African Lyon leo Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam baada ya mazoezi ya siku mbili tu, juzi na jana kufuatia mgomo wa siku mbili wa wachezaji wake wakishinikiza kulipwa mishahara ya Novemba.
    Lakini Lwandamina aliihakikishia Bin Zubeiry Sports - Online jana kwamba wachezaji wake wamemuahidi kuweka kando matatizo yote na kuingia kwa nguvu zao zote kuwakabili Lyon.
    “Wachezaji wamenihakikishia kuacha nyuma matatizo yote na kuingia kwenye mchezo wa Ijumaa kwa nguvu zao zote,”alisema Lwandamina na kuongeza; “Matarjio yangu ni matokeo mazuri baada ya mshikamano huu wa wachezaji,”. 
    Wachezaji wa Yanga wameahidi kuweka pembeni matatizo yao ya mishahara na kuingia kwa nguvu moja katika mchezo dhidi ya African Lyon leo

    Mchezo huo utachezeshwa na refa Ludovic Charles kutoka mkoani Tabora, atakayesaidiwa na John Kanyenye wa Mbeya na Arnord Bugado wa Singida, wakati refa wa wa akiba atakuwapo Israel Nkongo wa Dar es Salaam.
    Yanga SC inahitaji ushindi katika mchezo wa leo ili kurejea kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na kuzidi kujiimarisha katika harakati za kutetea lake.
    Hata hivyo, mchezo huo unatarajiwa kuwa mgumu kwa Yanga kwa sababu tangu wacheze na JKT Jumamsi na kushinda 3-0 hawakuafanya mazoezi hadi Jumatano jioni na jana asubuhi kufuatia mgomo wa Jumatatu na Jumanne wachezaji wake wakishinikiza kulipwa yao iliyocheleweshwa ya mwezi Novemba.
    Mgomo huo ulizimwa baada ya kikao na Jumanne mchana kati ya uongozi na wachezaji baada ya ahadi ya malipo kufanyika kabla ya leo. Bado haijulikani kama wachezaji wa Yanga wataingia kwenye mechi ya leo baada ya kulipwa au la.
    Kwa sasa ni Simba SC ndiyo inayoongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 38 za mechi 16 ikiwazidi mabingwa hao watetezi kwa pointi mbili. 
    Ligi Kuu itaendelea Jumamosi wakati vinara Simba watakaposhuka dimbani kumenyana na JKT Ruvu Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam, mechi ambayo itachezeshwa na refa Hans Mabena wa Tanga, atakayesaidiwa na Omari Kambangwa wa Dar es Salaam na Khalfan Sika wa Pwani wakati Mbaraka Rashid wa Dar es Salaam atakuwa Mwamuzi wa Akiba na Kamishna atakuwa Tito Haule wa Morogoro.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu kesho ni kati ya Mbeya City na Toto Africans Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya, Kagera Sugar na Stand United Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, Ndanda FC na Mtibwa Sugar Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara, Maji Maji FC na Azam FC Uwanja wa Maji Maji, Songea na Mwadui FC dhidi ya Mbao FC Uwanja wa Mwadui Complex, Shinyanga.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA WAWEKA SHIDA PEMBENI .WAINGIA UWANJANI KWA NGUVU MOJA LEO KUINYOOSHA AFRICAN LYON Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top