• HABARI MPYA

    Thursday, December 29, 2016

    SIMBA WALEEE, YANGA WANAISOMA NAMBA...RUVU AFA 1-0

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    BAO pekee la kiungo Mohammed ‘Mo’ Ibrahim limetosha kuipa Simba ushindi wa 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
    Ni ushindi huo ambao unaifanya Simba SC ifikishe pointi 44 baada ya kucheza mechi ya 18 na kuendelea kuogoza Ligi Kuu kwa pointi nne zaidi ya mabingwa watetezi, Yanga SC.
    Mo aliyesajiliwa Simba SC msimu huu kutoka Mtibwa Sugar ya Morogoro, alifunga bao hilodakika ya 45 akimalizia krosi ya beki wa kulia, Janvier Besala Bokungu kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Simba ilipata bao hilo, baada ya kukosa mengine zaidi ya matatu ya wazi na pongezi zimuendee kipa chipukizi wa Ruvu Shooting, Bidii Hussein aliyeokoa hatari nyingi.
    Mfungaji wa bao pekee la Simba, Mohammed 'Mo' Ibrahim akikimbia kushangilia huku wachezaji wa Ruvu wakiwa wameduwaa  
    Wachezaji wa Simba wakimpomgeza Mohamed Ibrahim (kulia) baada ya kufunga
    Mohammed Ibrahim akifumua shuti kuifungia Simba bao pekee leo
    Beki wa Simba, Mohammed Hussein 'Tshabalala' akiuzuia mpira wa juu kiufundi
    Kiungo wa Simba, Muzamil Yassin akimuacha chini beki wa Ruvu Shooting

    Kwa mara nyingine na ya pili mfululizo leo kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog alimuanzisha mshambuliaji mpya Pastory Athanas aliyesajiliwa dirisha dogo kutoka Stand United peke yake mbele.
    Lakini ngome ya Ruvu ilifanikiwa kumdhibiti mchezaji huyo chipukizi mwenye kipaji.
    Omog alimchezesha kwa mara ya kwanza mshambuliaji mwingine mpya, Juma Luizio aliyesajiliwa kwa mkopo kutoka Zesco United ya Zambia ambaye kwa dakia chache alizocheza kipindi cha pili alionyesha yuko vizuri.
    Ruvu Shooting nayo ikiongozwa na viungo wakongwe waliowaji kuwika Simba SC na timu ya taifa, Taifa Stars, Jabir Aziz Stima na Shaaban Kisiga ‘Malone’ ilionyesha upinzani mkali, lakini ikashindwa kupata mabao.
    Washambuliaji wa kigeni, Laudit Mavugo kutoka Burundi na Frederick Blagnon kutoka Ivory Coast hawakuwepo hata benchi kwenye mxhezo huo.
    Kikosi cha Ruvu Shooting kilikuwa: Bidii Hussein, Abdul Mpambika, Yusuph Nguya, Damas Makwaya, Renatus Kasase, Baraka Mtuwi, Jabir Aziz, Shaaban Kisiga, Fully Maganga, Ismail Mohammed/Chande Magoja dk57 na Abrahman Mussa. 
    Simba: Daniel Agyei, Janvier Bokungu/Said Ndemla dk80, Jonas Mkude, Mohammed Hussein, Abdi Banda, Method Mwanjali, Shiza Kichuya/Mwinyi Kazimoto dk68, Muzamil Yassin, James Kotei, Pastory Athanas na Mohammed ‘Mo’ Ibrahim/Juma Luizio dk52.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA WALEEE, YANGA WANAISOMA NAMBA...RUVU AFA 1-0 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top