• HABARI MPYA

    Sunday, September 20, 2015

    NINAWAHURUMIA MAKIPA HAWA WA YANGA SC

    KATIKA miaka ya karibuni, angalau mwaka huu usajili wa Yanga SC umekuwa na uwiano mzuri mno wa wachezaji na nafasi.
    Ni aina ya usajili unaofanana na wa kitaalamu, tofauti na miaka iliyopita ilipoonekana kama klabu ilisajili bila kuzingatia uwiano wa nafasi.
    Katika nafasi saba za wachezaji wa kigeni, Yanga SC imesajili mabeki wawili, ambao ni Mbuyu Twite wa DRC na Vincent Bossou wa Togo, viungo watatu ambao ni Thabani Kamusoko wa Zimbabwe, Andrey Coutinho wa Brazil na Haruna Niyonzima wa Rwanda na washambuliaji wawili Donald Ngoma wa ZImbabwe na Amisi Tambwe wa Burundi.
    Mbuyu Twite anayeweza kucheza pia kama beki wa kati na kiungo, katika beki ya kulia yupo pamoja na mzalendo Juma Abdul.

    Bossou anasubiri benchi pamoja na Pato Ngonyani, wakati Kelivn Yondan na Nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’ wanaanza beki ya kati.
    Kamusoko anaanza kama kiungo mkabaji, wakati Said Juma ‘Makapu’ anasubiri. Na wakati mwingine Kamusoko hucheza kama kiungo wa juu, chini yake akicheza Makapu, au Salum Telela.
    Haruna Niyonzima anaanza kama kiungo mchezeshaji, wakati Telela anasubiri benchi na mara kadhaa amekuwa akiingia kipindi cha pili kwa msimu huu.
    Amissi Tambwe na Ngoma wanaanzishwa pamoja kama washambuliaji, wakati Malimi Busungu na Matheo Anthony Simon wanasubiri.
    Coutinho anasubiri benchi wakati Simon Msuva na Deus Kaseke au Godfrey Mwashiuya wanaanza kushambulia kutokea pembezoni mwa Uwanja. Beki ya kushoto Mwinyi Hajji Mngwali anaanza, wakati Oscar Joshua anasubiri- hao ni wazalendo watupu.
    Nafasi pekee ambayo wamelundikana wachezaji ni langoni- Yanga SC imesajili makipa wanne, ambao wote wamewahi kudakia timu ya taifa, Taifa Stars.
    Hao ni Ally Mustafa ‘Barthez’, Deo Munishi ‘Dida’, Mudathir Khamis na Benedicto Tinocco. Barthez amekuwa akianza na Dida anasubiri benchi, wakati Mudathir na Tinocco waliosajiliwa msimu huu, wote wanapanda jukwaani.
    Katika kikosi cha aina hii, hata kocha kichwa hakimuumi sana katika kupanga wachezaji wa kucheza, kwa sababu karibu kila nafasi ina wastani wa wachezaji wawili.
    Changamoto ambayo inamkabili kwa sasa kocha wa Yanga SC, Mholanzi Hans van der Pluijm ni kuhakikisha analinda vipaji vya nyota wote alionao kikosini.
    Karibu kila mchezaji wa Yanga SC ni wa kiwango cha kimataifa na katika timu yoyote ya Ligi Kuu hapa nchini si wa kukaa benchi- ila kwa kuwa wamekutana wakali watupu Jangwani, lazima wengine wasubiri.
    Tunashukuru msimu huu kutakuwa mashindano ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ni matumaini yetu si kwa Yanga SC, bali timu zote za Ligi Kuu zitawapa nafasi wachezaji wa benchi katika michuano hiyo.
    Sehemu moja tu ambayo wachezaji wake wanatia huruma ni langoni. Sijui ni namna gani pamoja na kuwepo kwa Kombe la TFF makipa wote wanne watadaka msimu huu.
    Kipa wa pili, Dida anaweza kupata nafasi ya kudaka, vipi Mudathir na Tinocco, mustakabali wao utakuwaje? Hapa watu lazima waombeane majanga, wengine waumie au wafungiwe ili na wao wapate nafasi. Nawahurumia. 
    Sisemi moja kwa moja kwamba wamekwenda kuua vipaji vyao Jangwani, bali wanakabiliwa na changamto kubwa sana ili kufufua ndoto zao za kuwa makipa bora nchini.
    Kwa kawaida ya timu zetu, zinaposajili mchezaji na akashindwa kupata nafasi ya kucheza, hazishughuliki naye. Zinaangalia anayecheza na kumlinganisha na wa timu nyingine.
    Haitakuwa ajabu Desemba tu katika dirisha dogo mmoja kati ya makipa wa benchi wa Yanga SC, au hata wote wakatemwa akasajiliwa kipa mwingine. Ndiyo maana ninasema ninawahurumia sana makipa wapya wa Yanga SC. Alamsiki.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: NINAWAHURUMIA MAKIPA HAWA WA YANGA SC Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top