• HABARI MPYA

    Monday, September 21, 2015

    SIMBA SC NOMA, FIFA SASA YAIAMURU ETOILE DU SAHEL KULIPA MAMILIONI YA OKWI MARA MOJA, VINGINEVYO WAMEKWISHA!

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka la Kimataifa (FIFA) limeifungulia kesi kwenye Kamati ya Nidhamu ya FIFA dhidi ya klabu ya Etoile Sportive du Sahel ya Tunisa kutokana na klabu hiyo kushindwa kuilipa klabu ya Simba SC ya Tanzania pesa za mauzo ya mchezaji Emmanuel Arnold Okwi, dola za Kimarekani 300,000 (Sh. Milioni 600).
    Kwa mujibu wa barua ya FIFA kwa Shirikisho la Soka Tunisia (FTF) ambayo nakala yake imetumwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), klabu hiyo inashitakiwa  kwa kuvunja kanuni kwa mujibu wa ibara ya 64 ya kanuni za nidhamu za FIFA (Fifa Disciplinary Code).
    Tovuti ya TFF, imeandika kwamba kwa kuzingatia hilo, agenda hii itakuwa kwenye kikao kijacho cha kamati ya nidhamu.
    Emmanuel Okwi amekuwa mchezaji mwenye faida kubwa kihistoria Simba SC

    Etoile Sportive du Sahel wametakiwa kulipa mara moja kiasi cha dola za kimarekani laki 300,000 na riba ya asilimia mbili (2%) kwa kila mwaka kama ilivyoelekezwa na maamuzi ya Jaji mmoja wa Kamati ya Nidhamu za Wachezaji Novemba 20, mwaka jana.
    Tangu wakati huo, TFF imekua likiwasiliana na FTF na FIFA kwa niaba ya klabu ya Simba amabye ni mwanachama wa TFF, bila mafanikio.
    Ikiwa klabu hiyo ya Tunisia itafanya malipo kwa klabu ya Simba na kupelekea ushahidi wa malipo kwa FIFA basi suala hilo litafutwa.
    Aidha, klabu hiyo iko kwenye hatari ya kushushwa daraja au kupokwa alama  kwenye ligi (League Point) iwapo haitalishughulikia suala hilo mara moja.
    Emmanuel Okwi (kushoto) akiichezea Etoile du Sahel

    SAKATA LA OKWI;
    Okwi alinunuliwa na Etoile Januari mwaka 2013 kwa dau la rekodi kwa klabu za Tanzania, dola 300,000, ingawa baada ya muda akaingia kwenye mgogoro na klabu hiyo ya Tunisia.
    Mtafaruku ulianza baada ya Okwi kuchelewa kurejea mjini Sousse mkoani Sahel baada ya ruhusa ya kwenda kuichezea timu yake ya taifa, Uganda.
    Okwi naye akadai Etoile walikuwa hawamlipi mishahara na kufungua kesi FIFA (Shirikisho la Soka la Kimataifa), ambayo mwisho wa siku alishinda kwa kuruhusiwa kutafuta timu nyingine ya kuchezea kulinda kipaji chake, wakati wa mgogoro wake na klabu ya Tunisia.
    Okwi akajiunga na SC Villa ya kwao, Kampala katikati ya mwaka 2013 na Desemba mwaka huo, akahamia Yanga SC. 
    Okwi akiwa na 'kigogo' wa Yanga SC, Mussa Katabaro wakati anawasili kujiunga na klabu hiyo
    Hata hivyo, Okwi akavunja Mkataba na Yanga SC Agosti waka jana, baada ya timu hiyo ya Jangwani kushindwa kumlipa dola za Kimarekani 60,000 kama ilivyokuwa katika Mkataba baina yao na kurejea klabu yake ya zamani, Simba.
    Na mapema Oktoba mwaka huu, SImba SC nayo ilimuuza Okwi  SonderjyskE FC ya Ligi Kuu ya Denmark ambako amesaini Mkataba wa miaka mitano.
    Okwi wakati anatambulishwa SonderjyskE FC ya Ligi Kuu ya Denmark baada ya kusaini Mkataba wa miaka mitano
    Hans Poppe akimkabidhi Okwi jezi ya Simba SC wakati anarejea kutoka Yanga SC

    HANS POPPE AFURAHIA NEEMA
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe amepokea kwa furaha taarifa hizo na amesema anaamini sasa haki yao itapatikana.
    "Ukweli ni kwamba ilifikia wakati tukakata tamaa, kabisa. Lakini sasa kwa hatua hii ya FIFA naamini hawa mabwana sasa watatulipa fedha zetu na litakuwa jambo zuri sana kwa wakati huu ambao klabu inahitaji fedha kutekeleza miradi mbalimbali ya kimaendeleo. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC NOMA, FIFA SASA YAIAMURU ETOILE DU SAHEL KULIPA MAMILIONI YA OKWI MARA MOJA, VINGINEVYO WAMEKWISHA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top