• HABARI MPYA

    Thursday, April 23, 2015

    DIAMOND: NAIPENDA YANGA SC SABABU YA NGASSA

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
    MWANAMUZIKI nyota Tanzania, Nassib Abdul ‘Diamond’ amesema kwamba kwa sasa anashabikia Yanga SC kwa sababu ya Mrisho Ngassa.
    Na Diamond amesema nchini Tanzania yeye hashabikii timu yoyote, bali anampenda mchezaji Mrisho Ngassa.
    “Mimi huwa nashabikia timu anayochezea Ngassa. Kwa hiyo sasa hivi nashabikia Yanga, ila Ngassa akihama, na mimi nitahamia timu atakayohamia yeye,”amesema Diamond.
    Diamond na Mrisho ni maswahiba na Ngassa naye amewahi kusema anapenda kusikiliza muziki wa Diamond tu.
    “Mimi huwa nasikiliza muziki wa Diamond tu. Huyo ndiye mwanamuziki ninayemkubali hapa Tanzania,” amewahi kusema Ngassa.
    Diamond (kulia) akiwa na swahiba wake Mrisho Ngassa (kushoto)

    Hata katika simu zake zote, Ngassa ameweka miito ya nyimbo za Diamond.
    Kuna uwezekano Ngassa akaondoka Yanga SC kufuatia kumaliza Mkataba wake Aprili 20, ingawa mwenyewe amekuwa mgumu kuweka bayana.
    “Kwa sasa sitaki kuzungumzia masuala ya Mkataba, nataka nimalize msimu kabisa ndiyo nianze mijadala ya Mkataba mpya. Mimi ni mchezaji niliyesajiliwa Yanga msimu huu. Nitamalizia msimu, baada ya hapo mengine yatafuata,”alisema Ngassa akizungumza na BIN ZUBEIRY juzi.
    Kuhusu uvumi kwamba amesaini timu ya Free State Stars ya Afrika Kusini, Ngassa alisema; “Nipo kwenye mazungumzo na timu tatu, ikiwemo hiyo Free State, nyingine ya Qatar na pia nimeletewa ujumbe kwamba AS Vita (ya DRC) na Etoile nao wananifuatilia. Ndiyo maana nasema acha nimalize msimu kwanza, sina papara,”amesema.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DIAMOND: NAIPENDA YANGA SC SABABU YA NGASSA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top