• HABARI MPYA

    Sunday, August 31, 2014

    MAMBO MATATU YA KUJIULIZA SAKATA LA OKWI, YANGA NA SIMBA…

    POPOTE utakapoona mkusanyiko wa mashabiki wa Simba na Yanga au wa klabu mojawapo pekee kati ya hizo, ukiusogelea utakutana mjadala mmoja tu unaendelea. Okwi, Okwi, Okwi.
    Ukitega vipindi vya michezo vya Televisheni na Redio nchini kwa sasa, mjadala mkubwa ni mmoja tu. Okwi, Okwi, Okwi.
    Kurasa za habari na makala pamoja na safu za uchambuzi za magazeti ya michezo, halikadhalika ni kuhusu Okwi tu. Hata kwenye mitandao yetu ya kijamii. Ni Okwi tu.
    Mwansoka wa kimataifa wa Uganda, Emmanuel Arnold Okwi kwa mara nyingine ameteka mijadala ya kimichezo nchini, kufuatia kujiunga kwake na Simba SC, huku Yanga SC wakidai bado wana mkataba naye.

    Jioni ya Alhamisi wiki hii (Agosti 28, 2014) Okwi alitangaza kurejea Simba SC kwa mkataba huru wa muda, akidai Yanga SC imesitisha mkataba naye pamoja na kumshitaki TFF.
    Okwi alisema ameamua kuomba kuichezea Simba SC kipindi hiki ambacho ana matatizo na Yanga SC ili kulinda kipaji chake, kwa kuwa hata FIFA haitaki mchezaji akae bila kucheza.
    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe alisema kwamba wamemsaini mchezaji huyo baada ya kupitia kwa kina suala lake na Yanga SC na kugundua haki ipo upande wa mchezaji.
    Poppe amesema wametuma jina la Okwi TFF wakiambatanisha na barua yake ya kuomba kusajiliwa na Simba SC na barua ya klabu yake hiyo kuvunja naye Mkataba.
    Yanga SC Ijumaa (Agosti 29, 2014) wakaibuka na kukana kuvunja naye Mkataba na kusema mshambuliaji huyo Mganda, amewahadaa Simba SC ambao wameingia mkenge.
    Wakasema wameandika barua Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuomba imfungie Okwi kucheza soka na kuifungia Simba SC pia kwa kumsajili mchezaji ambaye ana mkataba.
    Akizungumza katika Mkutano na Waandishi wa Habari mchana wa juzi, makao makuu ya klabu hiyo, makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Yanga SC, Yussuf Manji alisema kwamba anaipa TFF siku saba kutekeleza hayo.
    Manji alisema, iwapo TFF itashindwa kutekeleza hayo ndani ya siku hizo saba, wao watahamia Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) ambako kama hawatafanikiwa pia, watahamia Mahakama ya Usuluhishi ya Michezo (CAS).
    Manji alisema juzi asubuhi walituma malalamiko yao kimaandishi TFF na pia wanamdai Okwi fidia ya dola za Kimarekani 500,000 (Sh. Milioni 900) kutokana na kuvunja mkataba na wao.
    Mwenyekiti huyo amesema kwamba, kabla ya juzi katika malalamiko ya awali waliyotuma TFF, walitaka Okwi awalipe dola 200,000 (zaidi ya Sh. Milioni 340,000), lakini baada ya Simba kutangaza imemsajili, dau limepanda.
    Manji alisema kwamba Yanga haina ubaya na Simba, bali watani wao hao wa jadi, wamefanya vibaya kumsainisha mchezaji huyo bila kuwasiliana nao. 
    Amesema Yanga haitatetereka kwa kuondoka kwa Okwi, shida ni kwamba taratibu hazikufuatwa. 
    Ikumbukwe, Okwi alikuja Tanzania kwa mara ya kwanza mwaka 2009 kujiunga na Simba SC akitokea SC Villa ya Uganda.
    Alicheza Simba SC hadi Januari mwaka jana alipouzwa kwa dola za Kimarekani 300,000 (Sh. Milioni 500) Etoile du Sahel ya Tunisia.
    Etoile haikulipa fedha hizo Simba SC na baadaye ikaingia kwenye mgogoro na Okwi, aliyedai hakulipwa pia mishahara yake kwa miezi mitatu.
    Etoile, ilidai mchezaji huyo alikiuka mkataba wake kwa kuchelewa kurejea kujiunga na klabu baada ya ruhusa ya kwenda kuichezea timu yake ya taifa
    Kesi yake na Etoile FIFA ikiendelea, Okwi akaomba wakati mgogoro wao unaendelea, aruhusiwe kuchezea timu yoyote kulinda kipaji chake. FIFA ilimkubalia na kutoa kibali cha muda kumruhusu kujiunga na SC Villa.
    Akiwa SC Villa ndipo aliposaini Yanga SC Desemba mwaka jana na pamoja na mapingamizi yaliyoanzia ndani, na baadaye klabu yake, Etoile- lakini Okwi aliidhinishwa kuichezea timu hiyo ya Jangwani.
    Okwi aliichezea Yanga SC mechi 11 na kuifungia mabao matano- lakini kuelekea mechi tano za mwisho za Ligi Kuu msimu uliopita akaingia kwenye mgogoro na klabu hiyo.
    Okwi alisusa kushinikiza amaliziwe fedha zake za usajili na mgogoro wao umeendelea huku mchezaji huyo akiwa amesusa tangu Machi, miezi minne tu baadaye tangu asajiliwe.
    Vikao kadhaa vilifanyika baina ya Okwi na Yanga SC tangu hapo kutafuta suluhu ya suala hilo, lakini mwisho wake umekuwa si mzuri.
    Pamoja na maelezo ya pande zote tatu, Yanga SC, Okwi na Simba- barua ambazo Yanga SC walipeleka TFF zinatoa undani zaidi wa sakata hili.
    Kwa kiasi kikubwa suala linajadiliwa kishabiki zaidi na walio wengi hadi kwenye vyombo vya habari, ambavyo inafikia wakati vinasahau vilikuwa vinaripoti nini awali kuhusu Yanga na mchezaji huyo kabla ya haya yaliyotokea.
    Yanga SC baada ya kuleta Wabrazil wawili, Geilson Santana ‘Jaja’ na Andery Coutinho ilikuwa katika msamiati wa imuache nani kati ya Mganda mwingine, Hamisi Kiiza na Okwi.
    Sijui ni kwa sababu Kiiza ndiye aliyeanza kurejea Dar es Salaam na kujiunga na timu kambini, au vipi lakini mwishoni kocha Mbrazil, Marcio Maximo akaamua atabaki na Diego wa Kampala.
    Baadaye viongozi wa Yanga SC wakaanza kutilia shaka uwezo wa Jaja, na kuanza kumshawishi Maximo akubali kumtema Mbrazil mwenzake huyo, ili asajiliwe Okwi.
    Maximo aligoma na akatishia naye pia kuondoka, iwapo Jaja angetemwa, tena akisema mchezaji huyo hajui kupiga chenga kama Haruna Niyonzima, lakini ana uwezo wa kufunga na Toni Kroos.
    Yanga SC wakanywea kwa Maximo na kimsingi wakaridhia kumtema Okwi- na hata barua ambazo wameandika TFF, wanaomba Mkataba wao na mchezaji huyo usitambuliwe tena, uvunjwe bila Mganda huyo kulipwa chochote.
    Lakini Yanga SC pia wamedai kurejeshewa fedha zao za usajili ambazo Okwi amechukua, kurejesha mishahara ambayo mchezaji huyo amechukua kimakosa na kuilipa klabu fidia ya dola za Kimarekani 200,000 (zaidi ya Sh Milioni 340,000) kwa hasara aliyoitia klabu ikiwemo kuwakosesha ubingwa msimu uliopita.
    Klabu hiyo ya Jangwani pia imeomba mchezaji huyo na wakala wake Edgar Agaba ambaye pia ni Mwanasheria wafungiwe kujihusisha na masuala ya soka, kwa sababu kwa pamoja awali walikwishaingia kwenye mazungumzo na klabu ya Wadi Galde ya Misri wakati bado wana mkataba wa miaka miwili na Yanga SC.
    Baada ya malalamiko haya ya Yanga SC TFF, shirikisho hilo la soka nchini likawaandikia barua wote kuwaita kwenye kikao cha Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji kuanzia Septemba 6 hadi 8.
    Ikumbukwe dirisha kuu la usajili kimataifa ambalo linahusu wachezaji wa kigeni pia linafungwa Septemba 6, wakati TFF imepanga Okwi na Yanga wakutane kwenye Kamati hiyo kuanzia Septemba 6 hadi 8.
    Katika mlolongo wa kesi hii, kuna mambo ambayo hayajawekwa wazi na Simba na Okwi mwenyewe kabla ya kufikia uamuzi wa kuingia Mkataba huo.
    Wakati Yanga SC inamsajili Okwi, ilitangaza hadharani imeingia naye Mkataba wa miaka miwili na nusu- maana yake Mkataba huo upo hai sasa.
    Lakini utaona katika sakata hili Yanga SC wameomba Mkataba uvunjwe bila mchezaji kulipwa chochote, bali yeye ndiye ailipe klabu hiyo.
    Pamoja na barua ya kumuita kwenye kikao mwezi ujao, TFF pia ilimpa Okwi nakala za barua za malalamiko ya Yanga SC dhidi yake.
    Bila shaka, Okwi baada ya kuzipitia barua hizo akafikia uamuzi wa kwenda Simba SC- huku akiandika barua za maombi ya kucheza ili kunusuru kipaji chake wakati kesi hiyo ikiendelea.
    Hapo hapo, kesi ya Okwi na Etoile haijamalizika na malalamiko ya klabu hiyo ya Tunisia hayapishani sana na ya Yanga SC.
    Sitaki kuingilia uhuru wa Kamati ya Sheria Maadili na Hadhi za Wachezaji itakayokutana baadaye kujadili kesi hiyo, lakini nina maswali matatu nataka kuchangia na wasomaji wangu.

    1. Yanga SC ilipomsajili Okwi huku Etoile inadai bado ni mchezaji wao, je ilikwenda kuuliza kwa klabu hiyo ya Tunisia kama inaweza kufanya hivyo?
    2. Yanga SC baada ya kuomba TFF mkataba wao na Okwi usitambuliwe bila mchezaji kulipwa chochote bali wao kulipwa fidia, inawezaje kusema huyo bado mchezaji wao halali?
    3. Okwi atatokea katika usajili wa Simba na Yanga. Lakini Yanga itakuwa na wachezaji sita wa kigeni, mmoja zaidi ya mahitaji ya kanuni, wakati Simba itakuwa na wachezaji watano tu kwa mujibu wa kanuni. Je, TFF itamkata mchezajii gani kwenye usajili wa Yanga kati ya Okwi, Coutinho, Jaja, Haruna Niyonzima, Mbuyu Twite na Kiiza? Leo naomba niishie hapa, kunako majaaliwa tutaendelea Jumatano. Alamsiki. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAMBO MATATU YA KUJIULIZA SAKATA LA OKWI, YANGA NA SIMBA… Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top