• HABARI MPYA

    Thursday, March 12, 2009

    JAMANI AJIRA SIMBA SC, CHANGAMKIENI...

    Mwenyekiti wa Simba SC inayotafuta wafanyakazi, Hassan Dalali (kulia) akipokea jezi kutoka kwa bosi wa Vodacom, wadhamini wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Emillian Rwejuna.


    MWENYEKITI wa kamati ya usaili katika klabu ya Simba, Ayoub Semvua, amewaomba wanachama wa klabu hiyo wenye sifa kujitokeza kuomba nafasi ya Katibu Mkuu wa klabu hiyo.
    Amesema kuwa maoni ya kuomba ukatibu mkuu wa klabu hiyo yalianza kupokewa jana kwenye makao makuu ya klabu.
    “Mtu yeyote mwenye sifa anatakiwa kuja na kuomba nafasi hiyo,” alisema Semvua.
    Sifa za mwombaji ni pamoja na kuwa mwanachama hai wa Simba, uzoefu kuanzia wilaya hadi Taifa, heshima na uadilifu, umri usiopungua miaka 30, awe na elimu kuanzia kidato cha nne hadi elimu ya juu.
    Sifa nyingine ni kuwa na taaluma ya mpira wa miguu, ajue kuandika na kuzungumza kwa ufasaha lugha ya Kiswahili na Kiingereza.
    Kamati hiyo imepewa siku 21 iwe imeshapata majina matano ya wanachama wenye sifa na kuyawasilisha kwa kamati ya utendaji, ambayo yatachujwa hadi kupatikana mmoja mwenye sifa ambaye ndiye atakayekuwa katibu mkuu wa klabu hiyo.
    Ifikapo Aprili Mosi, Simba itakuwa imeshakamilisha zoezi la kumpata katibu mkuu mpya.
    Katibu Mkuu wa sasa wa Simba, Mwina Kaduguda, ameshatangaza kuwa ataendelea kuongoza klabu hiyo hadi Desemba 29, siku ambayo anatarajiwa kumaliza muda wake wa uongozi kwa mujibu wa katiba ya klabu hiyo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: JAMANI AJIRA SIMBA SC, CHANGAMKIENI... Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top