• HABARI MPYA

    Monday, October 28, 2013

    MALINZI AMSAMEHE WAMBURA NA KUMFUTIA ADHABU YA TENGA...ASAMEHE PIA WOTE WALIOKUWA WAMEFUNGIWA NA TFF 'ILIYOEKSPAYA'

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    RAIS mpya wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ametoa msameha kwa wanachama wote wa shirikisho hilo waliofungiwa chini ya Utawala wa rais aliyemaliza muda wake, Leodegar Tenga, isipokuwa tu wale ambao adhabu zao zinatokana na makosa ya rushwa na kupanga matokeo. 
    Maana yake- Michael Richard Wambura aliyekwama kabisa kugombea nafasi yoyote chini ya utawala wa Tenga, sasa yuko huru kugombea au kuteuliwa kwa nafasi yoyote ya uongozi katika soka ya Tanzania.
    Nasamehe wote, tuanze upya; Jamal Malinzi akitangaza msamaha kwa wote waliofungiwa jana. Kulia ni Makamu wake, Walace Karia

    Akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi katika uchaguzi uliomalizika usiku wa manane jana ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam, Malinzi aliiagiza Sekretarieti ya TFF chini ya Katibu wake, Angetile Osiah mara moja kuandika barua za misamaha kwa wote wanaotumikia adhabu za utawala wa Tenga.
    “Hata rais wa nchi anapoingia madarakani huwa anatoa misamaha, nami nachukua fursa hii kuomba ridhaa yenu Wajumbe, kwa kuwa huu ni uongozi mpya, basi tufungue ukurasa mpya, nipeni ridhaa yenu, watu wote waliofungiwa chini ya utawala uliomaliza muda wake, wasamehewe tuanze upya. Isipokuwa wale tu ambao adhabu zao zinatokana na rushwa na upangaji matokeo,”alisema Malinzi.
    Malinzi alisema muda si mrefu atakutana na Kamati yake ya Utendaji kujipanga na amewataka wajumbe wote kujiandaa kwa hilo.
    Kwa upande wake, Tenga pamoja na kumpongeza Malinzi, aliahidi kumkabidhi ofisi Jumamosi ijayo. 
    Malinzi ameshinda Urais wa TFF baada ya kupata kura 72, dhidi ya 52 za mpinzani wake Athumani Jumanne Nyamlani.
    Katika uchaguzi huo uliofanyika kwenye ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam, Walace Karia alifanikiwa kushinda nafasi ya Makamu wa Rais kwa kupata kura 67 akiwashinda Nassib Ramadhani kura 52 na Imani Madega sita.   
    Kwa upande wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji walioshinda ni Kalilo Samson (Kanda namba 1- Geita na Kagera) aliyepata kura 102 za ndiyo na 17 za hapana. Kanda namba 2- Mara na Mwanza, mshindi ni Vedastus Lufano aliyepata kura 51 dhidi ya Jumbe Odessa Magati (11), Mugisha Galibona (24), na Samwel Nyalla (39).
    Epaphra Swai ndiye mshindi wa Kanda namba 3- Shinyanga na Simiyu kwa kura 63 dhidi ya Mbasha Matutu aliyepata 61. Kanda namba 4- Arusha na Manyara mshindi ni  Omali Walii Ali aliyepata kura 53 dhidi Elley Mbise (51), Ally Mtumwa (19).
    Kanda namba 4- Kigoma na Tabora, mshindi ni Ahmed Idd Mgoyi aliyepata kura 92 dhidi ya 28 za Hamisi Yusuf Kitumbo.
    Ayubu Nyaulingo na Blassy Mghube Kiondo ameshinda Kanda namba 6- Katavi na Rukwa kwa kura 73 dhidi ya Ayubu Nyaulingo aliyepata 52. Ayoub Shaibu Nyenzi ndiye mshindi wa Kanda namba 7- Iringa na Mbeya kwa kupata kura 59 na kuwapiku David Samson Lugenge (8), John Exavery Kiteve (12) na Lusekelo Elias Mwanjala (46).
    Kanda namba 8- Njombe na Ruvuma inawakilishwa na James Patrick Mhagama aliyepata kura 93 dhidi ya 31 za Kapteni mstaafu Stanley William Lugenge. Athuman Kingombe Kambi ndiye mshindi wa Kanda namba 9- Lindi na Mtwara kwa kura 84 akiwazidi Francis Kumba Ndulane (30) na Zafarani Mzee Damoder (11).
    Hussein Zuberi Mwamba ametetea ujumbe wa Kanda namba 10- Dodoma na Singida kwa kura 63 akiwapiku Stewart Masima (58) na Charles Komba (4). Geofrey Irick Nyange ameshinda Kanda namba 11- Morogoro na Pwani akipata kura 78 dhidi ya Juma Pinto (26), Farid Nahdi (14), Riziki Juma Majala (5) na Twahil Twaha Njoki (2).
    Kanda namba 12- Kilimanjaro na Pwani, Khalid Abdallah Mohamed ndiye aliyeibuka kidedea kwa kura 69 dhidi ya 54 za mpinzani wake Davis Elisa Mosha.  Kidao Wilfred Mzigama ameshinda Kanda namba 13- Dar es Salaam kwa kupata kura 60 dhidi ya wapinzani wake Muhsin Said Balhabou (50), Omar Isack Abdulkadir (10) na Alex Crispine Kamuzelya (4).
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MALINZI AMSAMEHE WAMBURA NA KUMFUTIA ADHABU YA TENGA...ASAMEHE PIA WOTE WALIOKUWA WAMEFUNGIWA NA TFF 'ILIYOEKSPAYA' Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top