• HABARI MPYA

    Saturday, October 26, 2013

    YUSSUF BAKHRESA: WATANZANIA WAJIVUNIE AZAM TV YA WAZAWA, WATANZANIA WENZAO

    Na Mahmoud Zubeiry, Tazara
    MMOJA wa Wakurugenzi wa Azam Media Group, Alhaj Yussuf Said Salim Awadh Bakhresa amesema kwamba Watanzania wanapaswa kujivunia Televisheni ya kimataifa ya Azam TV, kwa sababu ni mali ya Watanzania wenzao na wazawa.
    Akizungumza katika mahojiano maalum na BIN ZUBEIRY jana eneo la Tazara zilizopo ofisi za Azam Media, barabara ya Nyerere, Dar es Salaam, Yussuf alisema kwamba wazo la kuanzisha Azam TV aliliwasilisha yeye katika ukoo wao kwa lengo la kuwanufaisha Watanzania.
    Yussuf Bakhresa kushoto akielekezwa jambo na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media, Rhys Torrington alipotembelea ofisi hizo jana barabara ya Nyerere, Dar es Salaam

    “Hili lilikuwa wazo langu, na nashukuru Mungu ndugu zangu, kaka zangu, na wazazi wangu wote wakaafiki, maana yake lilikuwa wazo zuri na lenye manufaa kwa Watanzania kwa ujumla.
    Soka ya Tanzania inanufaika kwa namna zaidi ya moja au mbili, kwanza klabu zinapata fedha za haki ya matangazo ya Televisheni, ambayo Azam TV imenunua. Lakini pia kitendo cha kuonyesha mechi za Ligi Kuu ni fahari kwa ligi yetu na inaongeza hamasa na mapenzi ya Watanzania kwa soka yao,”.
    “Yapo maeneo mengi sana ambayo tulizingatia katika kuleta Azam TV, lakini kubwa ni unaweza kuona hii itajenga hamasa kubwa katika soka yetu ukiondoa klabu kunufaika kifedha,”alisema Yussuf.
    Kuhusu huduma rasmi za Azam TV, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media, Rhys Torrington alisema kwamba zitaanza mwezi ujao.
    Yussuf Bakhresa jana alikuwa ana kikao kizito na Torrington


    Kikao kilifanyika ofisini kwa Torrington

    CEO wa Azam Media ni msikivu

    Bosi rafiki; Torrington na Yussuf wanaelewana sana

    Mwanzo mzuri; Azam TV imepokewa vizuri na Watanzania

    Torrngton akimsikiliza kwa makini Yussuf

    Torrington akimuonyesha Yussuf ofisi za Azam Media

    Umejitahidi mashaallah! Yussuf akistaajabu uzuri wa ofisi za Azam Media

    “Tutafungua milango ya Azam TV rasmi katikati ya Novemba kwa huduma ya chaneli 35 ambazo watu wajionea bure na uzinduzi utafanyika Novemba hiyo hiyo,”alisema.
    Torrington alisema kwamba king’amuzi cha Azam TV kitauzwa kwa Sh. 95,000 pamoja na dishi lake na pia mteja kupatiwa huduma za kufungiwa na kuunganishiwa bure nyumbani kwake.
    Alisema malipo ya mwezi yatakuwa ni Sh. 12,500 tu na mteja atapata chaneli zaidi ya 50 katika king’amuzi cha Azam TV.
    Alisema Azam TV pekee kwa kuanzia itakuwa na chaneli tatu ambazo ni Azam One itakayohusu habari za Afrika na zaidi za Kiswahili, Azam Two ambayo itakuwa ya kimataifa yenye vipindi mbalimbali duniani, na baadhi vya Kiswahili na Sinema Zetu itakayokuwa ikionyesha sinema za Kitanzania kwa saa 24 kila siku.
    Alisema Azam TV imedhamiria kutoa huduma bora kwa bei nafuu kwa kuzingatia hali halisi ya Mtanzania na amewataka wananchi kujitokeza kununua ving’amuzi vya Azam TV mwezi ujao, mara tu huduma hizo zitakapoanza rasmi.
    Kwa sasa, Azam TV iliyonunua haki za matangazo ya Televisheni ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inaonyesha michezo ya ligi hiyo kupitia Televisheni ya Taifa, TBC1.
    “Mkataba wa sasa kati yetu na TBC1 unaisha mwishoni mwa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu na kuanzia mzunguko wa pili, Watanzania watapata moja kwa moja huduma za Azam TV kupitia ving’amuzi vyao watakavyonunua kuanzia mwezi ujao.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YUSSUF BAKHRESA: WATANZANIA WAJIVUNIE AZAM TV YA WAZAWA, WATANZANIA WENZAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top