• HABARI MPYA

    Friday, October 25, 2013

    DHAIRA AKABIDHIWA KWA WANAJESHI WAMPONYE HARAKA AIKABILI AZAM JUMATATU TAIFA

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    KIPA namba moja wa Simba SC, Abbel Dhaira amekwenda kufanyiwa uchunguzi asubuhi hii katika hospitali Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), kitengo cha wanamaji kutokana na matatizo ya msuli wa nyuma ya shingo. 
    Daktari wa Simba SC, Yassin Gembe ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba Dhaira amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya msuli wa nyuma ya shingo tangu kwenye mechi dhidi ya Yanga Jumapili ambayo alifungwa mabao matatu katika sare ya 3-3.
    Abbel Dhaira

    “Kama utakumbuka katika mechi dhidi ya Yanga alitibiwa tibiwa wakati mchezo unaendelea, ni kutokana na matatizo hayo hayo, kwa hivyo sasa hivi nakwenda naye akafanyiwe uchunguzi,”amesema Gembe asubuhi hii. 
    Dhaira alitoka dakika ya 35 juzi katika mchezo dhidi ya Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani, Tanga baada ya kugongana na mshambuliaji wa Coastal Union, Haruna Moshi ‘Boban’, timu hizo zikitoka sare ya 0-0.
    Kipa huyo alisema alipata maumivu madogo kichwani, ambayo anaamini hayatamuweka nje ya uwanja kwa muda mrefu na anataraia kucheza Jumatatu mechi nyingine ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Jumatatu dhidi ya Azam Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Simba SC imerejea Dar es Salaam jana na tayari ipo kambini kwake, Bamba Beach, Kigamboni ikiendelea na maandalizi ya mechi dhidi ya Azam.
    Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na ushindani mkali kutokana na timu hizo kukabana kileleni, zote zikiwa na pointi 20 sawa na Mbeya City baada ya mechi 10, lakini Simba SC inaizidi Azam wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: DHAIRA AKABIDHIWA KWA WANAJESHI WAMPONYE HARAKA AIKABILI AZAM JUMATATU TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top