• HABARI MPYA

    Tuesday, November 03, 2020

    YANGA SC YAPANDA KILELENI LIGI KUU LICHA YA KULAZIMISHWA SARE YA 0-0 NA GWAMBINA, MISUNGWI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    VIGOGO, Yanga SC wamepanda kileleni mwa Ligi Kuu ya Tanzania Bara licha ya sare ya bila kufungana na wenyeji, Gwambina FC jioni ya leo Uwanja wa Gwambina, wilayani Misungwi mkoani Mwanza.
    Kwa sare hiyo, Yanga SC inayofundishwa na Mrundi, Cedric Kaze inafikisha pointi 23, moja zaidi ya Azam FC baada ya kila timu kucheza mechi tisa.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Biashara United wamelazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na KMC Uwanja wa Karume, Musoma mkoani Mara.


    Lenny David Kissu alianza kuwafungia wenyeji dakika ya tano tu kabla ya Lusajo Mwaikenda kuisawazishia KMC kwa penalti dakika ya 55. 
    Mwisho wa mchezo, kocha Fulgence Novatus wa Gwambina alilalamika refa Hussein Athumani wa Katavi aliyekuwa anasaidiwa na Abdulaziz Ally wa Arusha na Edgar Lyombo wa Kagera kukataa bao lao halali lililofungwa na Nahodha wao, Jacob Massawe kipindi cha kwanza kwa madai mfungaji alikuwa ameotea.
    Kwa sare hiyo, Biashara United wanafikisha pointi 17 baada ya kucheza mechi 10, wakiwazidi pointi moja mabingwa watetezi, Simba SC ambao hata hivyo wana mechi mbili mkononi, wakati KMC inabaki nafasi ya tano ikifikisha pointi 15 za mechi 10.
    Ligi Kuu Tanzania Bara itaendelea kesho kwa mechi tatu, Simba SC na Kagera Sugar Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, Namungo FC na JKT Tanzania Uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Pwani na Mwadui FC na Ruvu Shooting Uwanja wa Mwadui Complex, Shinyanga.
    Kikosi cha Gwambina kilikuwa; Ibrahim Isihaka, Revocatus Richard, Amos Kadikilo, Salum Kipaga, Baraka Mtui, Novaty Lufunga, Meshack Mwamita, Yussuf Kagoma, Jimson Mwanure/Rajabu Rashid dk90, Jacob Massawe na Rajab Athumani.
    Yanga SC; Metacha Mnata, Paul Godfrey ‘Boxer’/Farid Mussa dk76, Yassin Mustapha, Abdallah Shaibu ‘Ninja’, Said Juma ‘Makapu’, Zawadi Mauya, Abdulaziz Makame, Tuisila Kisinda, Waziri Junior/Michael Sarpong dk58, Yacouba Sogne/Ditram Nchimbi dk76 na Deus Kaseke.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC YAPANDA KILELENI LIGI KUU LICHA YA KULAZIMISHWA SARE YA 0-0 NA GWAMBINA, MISUNGWI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top