• HABARI MPYA

    Thursday, August 16, 2018

    KUZIONA YANGA SC NA USM ALGER JUMAPILI SH 3,000 TU…MAKAMBO LIVE KWA MARA YA KWANZA TAIFA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIINGILIO cha chini katika mchezo wa Kundi D Kombe la Shirikisho Afrika baina ya wenyeji, Yanga SC dhidi ya U.S.M. Alger ya Algeria Jumapili Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam ni Sh. 3,000.
    Hayo yamesemwa na Ofisa Habari wa klabu ya Yanga SC, Dissmas Ten leo alipozungumza na Waandishi wa Habari leo makao makuu ya klabu, makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam.
    Ten amesema 3,000 itakuwa ni kwa majukwaa ya mzunguko, wakati watakaoketi VIP B na C watalipa Sh. 7,000 na VIP A itakuwa Sh.10,000.

    Mshambuliaji mpya, Heritier Makambo ataanza kucheza Jumapili baada ya kupatiwa leseni na CAF

    Mchezo huo utachezeshwa na Jackson Pavaza atakayepuliza filimbi akisaidiwa Matheus Kanyanga na David Tauhulupo Shaanika wote kutoka Namibia.
    Yanga SC ambayo itajaribu kusaka ushindi wa kwanza katika mechi zake za Kundi D Jumapili baada ya sare moja na kufungwa mechi tatu za awali, inatarajiwa kuwasili kesho kutoka Morogoro ilipokuwa imeweka kambi kwa wiki mbili.
    Yanga SC Ilianza michuano hiyo kwa kuchapwa mabao 4-0 na U.S.M. Alger nchini Algeria kabla ya kuja kutoa sare ya 0-0 na Rayon mjini Dar es Salaam na baadaye kwenda kufungwa mfululizo na Gor Mahia, 4-0 nchini Kenya na 3-2 Tanzania.
    Mchezo wa Jumapili safu ya ushambuliaji ya Yanga itaongezewa nguvu na mshambuliaji mpya, Heritier Makambo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ambaye amepatiwa leseni na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
    Kocha Mkongo wa Yanga, Mwinyi Zahera anatarajiwa kuwa kwenye benchi la timu kwa mara ya kwanza tangu aajiriwe miezi miwili iliyopita.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KUZIONA YANGA SC NA USM ALGER JUMAPILI SH 3,000 TU…MAKAMBO LIVE KWA MARA YA KWANZA TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top