Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM
KOCHA Mkuu wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mholanzi Mart Nooij amesema katika mchezo wa keshokutwa wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Benin atatoa kipaumbele kwa wachezaji warefu kwenye kikosi chake.
Kocha huyo wa zamani wa Ethiopia na Msumbiji ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba atafanya hivyo kwa sababu wapinzani wao, Benin kikosi chao kinaundwa na wachezaji warefu zaidi.
Nooij amesema kwamba lengo lake ni kuona kunakuwa na mapambano sawa katika kuwania mipira ya juu. “Itakuwa tofauti na kupanga wachezaji wafupi wengi, ambao wanaweza kuwapa wepesi Benin katika kushinda mipira mingi ya juu,”amesema.
Aidha, Nooij amesema katika mchezo huo atatumia mabeki watatu wa kati, ili kuwa na ukuta mgumu, mmoja wao akicheza kama kiungo mkabaji ili kuwapunguzia wenzake majukumu.
Amesema mpango huo unakuja kufuatia makosa yaliyofanywa na timu yake katika mechi ya mwisho dhidi ya Burundi ambayo ndani ya dakika 15 za kwanza walijikuta wanafungwa mabao mawili ya haraka haraka dakika ya kwanza na 12.
Kwa ujumla, tangu ametua Stars Nooij ameiongoza Stars katika mechi nane na kati ya hizo, ameshinda mbili amefungwa tatu na kutoa sare tatu na katika mechi zote hizo nyavu za Stars zimetikiswa mara 12, huku yenyewe ikifunga mabao tisa.



.png)
0 comments:
Post a Comment