MSHAMBULIAJI wa Paris Saint-Germain, Zlatan Ibrahimovic amegoma kujiunga na klabu za Ligi Kuu ya England kabla ya kustaafu soka.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 33, ambaye amecheza Ligi za Sweden, Uholanzi, Italia, Hispania na Ufaransa, amekuwa akitakiwa na klabu za England lakini mpango huo umekwama baada ya kukataa kwake.
Akiwa katika msimu wake wa tatu PSG, Ibrahimovic amesema kwamba anataka kubaki na mabingwa hao wa Ligue 1 na hatacheza Ligi Kuu England.
Alipoulizwa kama atachezea klabu ya England siku moja katika mahojiano na The Guardian, mshambuliaji huyo wa zamani wa Barcelona amesema: "Hapana. Nafurahia mjini Paris. Naiheshimu Ligi Kuu.
"Ni moja ya ligi bora duniani na hakuna ligi nyingine inayovutia hisia ya vyombo vya habari kama hii. Lakini nafurahi nimecheza ligi nyingi tofauti,".
Mshambuliaji huyo wa Sweden aliwahi kufanya majaribio Arsenal wakati anachezea Malmo ya nchini mwao akiwa kinda, lakini hakuivutia timu ya Arsene Wenger wakati huo.
Ibrahimovic amesema: "Leo, Wenger anasema ilikuwa ni kutoelewana. Lakini sikupenda kuambiwa kudhihirisha uwezo wangu. Nafahamu ni mzuri kiasi cha kutosha. Sihitaji kukuonyesha. Ikiwa unanifahamu au la.
"Nakumbuka nilikuwa katika ofisi ya Wenger na unaweza kusema alikuwa bosi. Alikuwa Wenger! Lakini sifikirii nilikuwa karibu (kusaini). Nilikwenda Ajax siku iliyofuata,"amesema.



.png)
0 comments:
Post a Comment