• HABARI MPYA

    Friday, January 08, 2016

    SIMBA SC KUIVAA MTIBWA SUGAR NUSU FAINALI, YANGA KUMENYANA NA URA

    Na Princess Asia, ZANZIBAR
    SIMBA SC itakutana na Mtibwa Sugar katika Nusu Fainali ya Kombe la Mapinduzi Jumapili, Uwanja wa Amaan, Zanzibar, wakati URA ya Uganda itamenyana na Yanga SC.
    Hiyo inafuatia Simba SC kumaliza kileleni mwa Kundi A baada ya leo kuifunga JKU 1-0 katika mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi ya michuano hiyo.
    Bao pekee la mabingwa hao watetezi, limefungwa na kiungo Jonas Gerald Mkude dakika ya 65, akimalizia krosi ya beki Mrundi, Emery Nimubona kutoka upande wa kulia.
    Simba SC ingeweza kuondoka na ushindi mkubwa leo kama wachezaji wake wangetumia nafasi walizopata tangu kipindi cha kwanza.
    Jonas Mkude akikimbia kushangilia baada ya kuifungia Simba SC bao pekee leo 

    Mshambuliaji Mkenya Paul Raphael Kiongera alikaribia kufunga dakika ya 12 kama si kupiga vibaya shuti lake akiwa ndani ya 18, kufuatia krosi ya mshambuliaji Mganda, Hamisi Kizza.
    Kizza naye alichelewa kuunganisha krosi ya winga Mganda mwenzake, Brian Majwega dakika ya 24, wakati Kiongera alidondoka na kushindwa kuunganisha krosi Kizza dakika ya 44.
    Sekunde chache kabla ya mapumziko, almanusra JKU wapate bao kama si kipa wa Simba SC, Peter Manyika kudaka shuti la mpira wa adhabu la Khamisi Makame.
    Kiungo Said Hamisi Ndemla alipiga pembeni dakika ya 60 akiwa amebaki na kipa na Mohammed Abrahman kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Ibrahim Hajib.
    Mbarouk Fakhi aliikosesha JKU bao la kusawazisha dakika ya 80 baada ya kupiga juu akiwa ndani ya boksi, kufuatia pasi nzuri ya Khamis Khamis.
    Kutoka Kundi A, JKU na Jamhuri zote zinaaga, huku Simba SC na URA zikitinga Nusu Fainali, wakati Kundi B Azam FC na Mafunzo zimetolewa, huku Yanga na Mtibwa wakisonga mbele.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Peter Manyika, Emery Nimubona, Brian Majwega/Joseph Kimwaga dk76, Abdi Banda, Hassan Isihaka, Jonas Mkude, Awadh Juma/Mwinyi Kazimoto dk46, Said Ndemla, Paul Kiongera/Ibrahim Hajib dk46, Peter Mwalyanzi/Mohammed Fakhi dk76 na Hamisi Kizza/Danny Lyanga dk46.
    JKU; Mohammed Abrahman, Ponsiana Malik Jose, Abdallah Waziri Suleiman, Khamis Abdallah Ali, Issa Haidari Dau, Khamis Said Khamis, Isamil Khamis Amour, Emmanuel Martin Joseph, Ally Vuai Hassan/Mbarouk Fakhi dk46, Khamis Mussa Makame/Feisal Abdallah dk71 na Mohammed Abdallah/Salum Salum dk71.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC KUIVAA MTIBWA SUGAR NUSU FAINALI, YANGA KUMENYANA NA URA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top