• HABARI MPYA

    Saturday, December 19, 2020

    WAZIRI BASHUNGWA ASEMA SERA YA MICHEZO NI HAI, ILA INAHITAJI MPANGO MKAKATI WA UTEKELEZAJI

    Na Shamimu Nyaki – WHUSM, DAR ES SALAAM
    WAZIRI wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa  amesisitiza kuwa Sera ya Michezo ya Mwaka 1995 inahitaji Mpango Mkakati kuitekeleza, ambapo amewasisitiza Wadau wa michezo kutoa maoni bora ya namna ya kutekeleza matakwa ya Sera hiyo kupitia Mpango Mkakati madhubuti.
    Bashungwa ameyasema hayo Desemba 19, 2020 Jijini Dar e salaam wakati alipofungua kikao cha kukusanya maoni kutoka kwa wadau wa michezo ikiwemo Vyama na Mashirikisho ya michezo kuhusu Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Michezo kwa miaka mitano , ambapo ameeleza kuwa lengo la kuwa na mpango huo ni kuboresha Sekta ya michezo ili ikue zaidi.
    “Mpango Mkakati huu utasaidia kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020- 2025 ambayo imesisitiza kukua kwa sekta ya michezo nchini ikiwemo ustawi wa timu za taifa” alisema Bashungwa.


    Waziri Innocent Bashungwa akifungua kikao cha kupokea maoni ya wadau kuhusu Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Michezo leo Jijini Dar es Salaam 

    Bashungwa ametumia nafasi hiyo kuliagiza Baraza la Michezo la Taifa kusimamia vyema Vyama vya Michezo na Mashirikisho katika kutekeleza majukumu yao huku akisitiza Utawala Bora ikiwemo kuheshimu Katiba zao, kufanya Uchaguzi kulingana na Sheria na kanuni pamoja na kujali maslahi ya Taifa katika kukuza michezo.
    Bashungwa ameeleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanazania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zitaendelea kushirikiana katika sekta hii ambapo amesema tayari Serikali zote mbili zimeanza maandalizi ya kushiriki Mashindano ya Olyimpiki ya mwaka 2021.
    Naye Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Abdallah Ulega amelisisitiza Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kukufanya kazi kulingana na matwaka ya dunia ya leo kwa kufuata Sheria na Kanuni za Baraza hilo ili lilete mafanikio ambayo yanatarajiwa katika sekta hiyo
    “Wawekezaji karibuni muwekeze katika Sekta hii ambayo ina vipaji vingi vinavyohitaji kuendelezwa ili visaide nchi katika michezo yote na kuitangaza”alisema Mhe.Bashungwa.
    Kwa upande wake Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt. Hassan Abbasi ameeleza kuwa Mpango Mkakati huo utasaidia   kutoa dira na kusaidia nchi kuwa na michezo ya vipaumbele itakayotangaza nchi vizuri.
    Vilevile, Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo Bw.Yusuph Singo amesema Idara imeanza kupokea maoni kutoka kwa wadau wa michezo katika maeneo mbalimbali ambapo kazi hiyo inatarajia kukamilika mwishoni mwa mwezi Desemba 2020.


    Baadhi ya Washiriki wa kikao cha kupokea maoni kuhusu Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Michezo kutoka kwa wadau wakiwemo Vyama na Mashirikisho ya Michezo kilichofanyika leo Dar es Salaam
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: WAZIRI BASHUNGWA ASEMA SERA YA MICHEZO NI HAI, ILA INAHITAJI MPANGO MKAKATI WA UTEKELEZAJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top