MSHAMBULIAJI wa Uruguay, Luis Suarez jioni ya leo amefunga mabao mawili timu yake hiyo ya taifa ikishinda 3-0 dhidi ya Oman katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa.
Nyota huyo wa Barcelona, ambaye atacheza mechi yake ya kwanza ya La Liga dhidi ya Real Madrid Oktoba 25, alifunga mabao hayo kipindi cha pili, la kwanza dakika ya 57 akimtungua kipa wa Oman, Ali Al Habsi ndani ya eneo la penalti.
Mchezaji huyo wa zamani wa Liverpool akafunga bao la pili dakika ya 67 akimtungua tena kipa huyo wa Wigan Athletic ya England, kabla ya Jonathan Rodriguez kufunga la tatu dakika za mwishoni. Baada ya kazi hiyo nzuri, Suarez alipumzishwa dakika ya 78, nafasi yake akiingia Christian Stuani.
Suarez bado anatumikia adhabu yake ya kutocheza mechi za mashindano baada ya kumng'ata Giorgio Chiellini wa Italia katika Kombe la Dunia Julai mwaka huu na anatarajiwa kuanza kazi Barcelona Oktoba 25, mechi yake ya kwanza ikiwa dhidi ya mahasimu, Real Madrid.


.png)
0 comments:
Post a Comment