• HABARI MPYA

    Saturday, December 28, 2013

    OKWI AMEANZA TABIA ZAKE ZA SIMBA NA ETOILE HATA YANGA SC?

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    UNAKUMBUKA ile tabia ya Emmanuel Okwi Simba SC kuchelewa kurejea mazoezini baada ya kuruhusiwa kwenda kwao Uganda kupumzika au kujiunga na timu ya taifa?
    Na si ndiyo tabia hiyo hiyo imechangia mgogoro wake na klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia? Basi ni kama anataka kuileta na katika klabu yake mpya, Yanga SC.
    Mshambuliaji huyo pamoja na Mganda mwenzake, Hamisi Kiiza ndiyo pekee ambao hawajarejea nchini kujiunga na timu kati ya wachezaji wa kigeni, baada ya ruhusa ya  muda mfupi kurejea nyumbani kwao.
    Ameanza kuwazingua na Yanga? Emmanuel Okwi hajarejea kujiunga na wenzake baada ya ruhusa ya mapumziko mafupi

    Yanga imeanza jana mazoezi chini ya kocha Freddy Felix Minziro, lakini Okwi na Kiiza hawakuwepo na taarifa zinasema hawajarejea nchini kabisa na haijulikani watakuja lini, wakati timu ipo kwenye maandalizi ya Kombe la Mapinduzi, michuano inayotarajiwa kuanza Januari 1, mwakani. 
    Mbali na Okwi na Kiiza, wachezaji wengine ambao hawajaripoti mazoezini ni kipa Juma Kaseja, ambaye na ruhusa maalum hadi Jumatatu na viungo Haruna Niyonzima, Nizar Khalfan, Hamisi Thabit na Hassan Dilunga ambao wote wanaumwa Malaria na Daktari Nassor Matuzya amethibitisha.
    Okwi alikuwa mchezaji wa Simba SC ya Dar es Salaam tangu mwaka 2010 hadi alipouzwa Etoile du Sahel ya Tunisia Januari mwaka huu kwa dola za Kimarekani 300,000, lakini mchezaji huyo akavurugana na klabu yake hiyo mpya wa tuhuma za kuchelewa kujiunga na timu baada ya kuruhusiwa kurejea Uganda kuichezea timu yake ya taifa.
    Inadaiwa, Okwi aliporejea Tunisia Etoile ikamkata mshahara na kumuamuru akafanye mazoezi na kikosi cha pili, lakini akagoma kufanya hivyo kurejea kupumzika kwao Uganda, akidai halipwi mishahara na kufungua kesi Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
    Baada ya Okwi kukaa bila kucheza kwa miezi sita, Shirikisho la Soka la Uganda (FUFA) lilimpigania aruhusiwe kurejea nyumbani kuichezea SC Villa ya huko ili kunusuru kiwango chake jambo ambalo alifanikiwa na mwezi huu amehamia Yanga.
    Tayari Yanga imepata ITC ya mchezaji huyo, lakini klabu yake ya zamani, Simba SC inapinga usajili wake kwenda Jangwani akitokea SC Villa kwa sababu ni mchezaji wa Etoile.
    Wakati huo huo, Etoile hadi sasa haijailipa Simba SC fedha zake za kumnunua mchezaji huyo na sakata lake limefikishwa FIFA, huku mustakabakali wa usajili wake Yanga ukiwa mikononi mwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
    Je, Okwi ndiyo amehamia Yanga na usumbufu wake aliokuwa anawafanyia Simba SC na Etlile du Sahel? 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OKWI AMEANZA TABIA ZAKE ZA SIMBA NA ETOILE HATA YANGA SC? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top