• HABARI MPYA

    Thursday, June 18, 2020

    SAMATTA ATOKEA BENCHI KIPINDI CHA PILI ASTON VILLA YALAZIMISHWA SARE 0-0 NA SHEFFIELD UNITED

    Na Mwandishi Wetu, BIRMINGHAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta ametokea benchi timu yake, Aston Villa ikilazimishwa sare ya 0-0 na Sheffield United Uwanja wa Villa Park Jijini Birmingham.
    Huo ulikuwa mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya England baada ya kurejea kufuatia mapumziko ya tangu katikati ya Machi kutokana na mlipuko wa maambukizi ya virusi vya corona duniani kote vinavyosababisha ugonjwa wa COVID 19.
    Na Samatta aliingia dakika ya 69 kuchukua nafasi ya kiungo Mholanzi, 21 Anwar El Ghazi, lakini hakuweza kuisaidia Aston Villa kupata ushindi nyumbani dhidi ya Sheffield United ambao walilalamika kunyimwa bao baada ya VAR kushindwa kufanya kazi.
    Mbwana Samatta na wachezaji wenzake wakiwa wamevalia fulana maalum za kupinga unyanyasi dhidi ya weusi 

    Kwa matokeo hayo, Aston Villa inabaki nafas ya 19 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 26 baada ya kucheza mechi 29, wakat Sheffield United inapanda kwa nafasi moja hadi ya sita ikifikisha pointi 44 baada ya kucheza mechi 29 pia.
    Wachezaji wa timu zote mbili walitokea uwanjani kupasha miili joto wakiwa wamevalia fulana maalum za kupinga unyanyasi dhidi ya weusi – na hiyo kufuatia tukio la Polisi Wazungu kumuua Mmarekani mweusi, George Floyd aliyekuwa ana umri wa miaka 46 Mei 25 huko Minneapolis, Minnesota baada ya kumkamata wakimtuhumu kukwepa kulipa bili zake dukani.
    Kikosi cha Aston Villa kilikuwa; Nyland, Konsa/El Mohamady dk76, Hause, Mings, Targett, Hourihane, Luiz, McGinn/Nakamba dk76, El Ghazi/Trezeguet dk69, Davis/Samatta dk69 na Grealish. 
    Sheffield United; Henderson, Basham, Egan, Robinson, Baldock, Berge/L Freeman dk69, Norwood, Lundstram, Stevens, McBurnie/Mousset dk80 na Sharp/McGoldrick dk69.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA ATOKEA BENCHI KIPINDI CHA PILI ASTON VILLA YALAZIMISHWA SARE 0-0 NA SHEFFIELD UNITED Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top