• HABARI MPYA

    Saturday, December 15, 2018

    MDOGO WAKE MSUVA AFUNGA MABAO MAWILI KMC YAIFANYIA BALAA ZITO TANZANIA PRISONS, YATAINDIKA 5-1 UHURU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni (KMC) leo imeiadhibu vikali Tanzania Prisons baada ya kuichapa mabao 5-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    Mabao ya KMC leo yamefungwa na Emmanuel Mvuyekure dakika ya 48 kwa penalti, Ally Msengi dakika ya 73, Sadallah Lipangile dakika ya 66 na James Msuva mawili dakika za 69 na 86, wakati bao pekee la Prisons limefungwa na Jumanne Elfadhili kwa penalti dakika ya 60.
    James Msuva ni mdogo wa kiungo mshambuliaji wa Difaa Hassan El-Jadidi ya Morocco, Simon Msuva ambaye amewahi kuchezea timu za vijana za Simba na Yanga kabla ya kujiunga na Mbao FC msimu uliopita katika Ligi Kuu na sasa yupi KMC.



    James Msuva amefunga mabao mawili leo KMC ikiichapa 5-1 Tanzania Prisons 

    Kwa ushindi huo mnono, KMC inayofundishwa na kocha Mrundi, Etienne Ndayiragijje inafikisha pointi 21 baada ya kucheza mechi 16 na kupanda hadi nafasi ya saba kutoka ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu.
    Prisons inayofundishwa na kocha Bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Abdallah Mohamed 'Bares' inaendelea kushika nafasi ya 19 katika ligi ya timu 20 kwa pointi zake 11 za mechi 17 sasa.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, Mbeya City imechapwa 2-0 na Lipuli FC nyumbani Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya. Lipuli FC inatoka nafasi ya 10 hadi ya nane kwa ushindi huo ikifikisha pointi 21 baada ya kucheza mechi 17 na Mbeya City inabaki nafasi ya tano kwa pointi zake 23 za mechi 16. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MDOGO WAKE MSUVA AFUNGA MABAO MAWILI KMC YAIFANYIA BALAA ZITO TANZANIA PRISONS, YATAINDIKA 5-1 UHURU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top