• HABARI MPYA

    Saturday, December 29, 2018

    AZAM YAANZA KUJITOA MBIO ZA UBINGWA, YACHAPWA 2-0 NA MTIBWA MANUNGU

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    TIMU ya Azam FC imeanza kujiondoa kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya kuchapwa mabao 2-0 na wenyeji, Mtibwa Sugar Uwanja Manungu, Turiani mkoani Morogoro.
    Kwa kipigo hicho, Azam FC inabaki na pointi zake 40 baada ya kucheza mechi 17, sasa ikizidwa pointi 10 na vinara Yanga SC ambao leo wameshinda 2-1 ugenini dhidi ya Mbeya City.
    Kwa ushindi huo uliotokana na mabao ya Kelvin Sabato dakika ya 15 na Ally Makarani dakika ya 81, Mtibwa Sugar inafikisha pointi 26 baada ya kucheza mechi 15 na kupanda hadi nafasi ya nne kutoka ya saba. 
    Mshambuliaji wa Azam FC, Obrey Chirwa akimiliki mpira mbele ya beki wa Mtibwa Sugar, Cassian Ponera leo Manungu

    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, African Lyon imelazimishwa sare ya 0-0 na Mwadui FC Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam, Lipuli FC pia imelazimishwa sare ya 0-0 na Ndanda FC Uwanja wa Samora mjini Iringa.
    Na Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani bao pekee la mshambuliaji wa mkopo kutoka Yanga, Emmanuel Martin dakika ya 53 limeipa Ruvu Shooting ushindi wa 1-0 dhidi ya Biashara United ya Mara.
    Mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu leo unafuatia Saa 1:00 usiku Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam, mabingwa watetezi, Simba SC wakiwakaribisha Singida United. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM YAANZA KUJITOA MBIO ZA UBINGWA, YACHAPWA 2-0 NA MTIBWA MANUNGU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top