• HABARI MPYA

    Saturday, May 20, 2017

    MAGURI AMUANDIKIA ‘BARUA YA WAZI’ KOCHA MAYANGA, AMUELEZEA MAFANIKIO YAKE OMAN

    Na Prince Akbar, DAR ES SALAAM 
    MSHAMBULIAJI Elias Maguri wa Dhofar ya Oman, amemtumia ‘barua ya wazi’ kocha wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Salum Mayanga kumuelezea mafanikio yake, japokuwa hamuhitaji kwa sasa kikosini kwake.
    Maguri ameandika ujumbe katika ukurasa wake wa Facebook ambao moja kwa moja utamgusa kocha Mayanga, ambaye jana tu ametaja kikosi cha wachezaji 23 wa Taifa Stars bila kumjumuisha mchezaji huyo wa zamani wa Simba, Ruvu Shooting na Stand United.
    “Napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya Ijumaa usiku tarehe 19/05/2017 kwa kutwaa ubingwa Ligi Kuu nchini Oman, kwani ni siku ambayo haitoweza kufutika katika historia yangu ya mpira,”amesema Maguri na kuongeza;
    Mshambuliaji Elias Maguri akifuraji na mchezaji mwenzake wa Dhofar ya nchini Oman 

    “Pia napenda kuwashukuru wale wote mliokua pamoja na mimi kwa kunisapoti kuhakikisha ninasonga mbele, pamoja na kutwaa ubingwa wa Ligi, napenda kuwajulisha pia siku ya tarehe 25 mwezi huu tunacheza fainali ya Kombe la Mfalme, na panapo majaaliwa tunaenda kunyanyua kwapa kwa mara nyingine,”amesema.
    Mfungaji huyo wa bao la kwanza la Taifa Stars katika sare ya 2-2 na Algeria Novemba 14 mwaka 2015 kwenye mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia, amesema kwa hiyo inaonyesha ni kiasi gani ndani ya msimu mmoja wa kucheza Oman amepata mafanikio makubwa.
    Jana Mayanga ameteua kikosi cha wachezaji 23 kitakachokwenda kuweka kambi Misri kujiandaa na mchezo wa kirafiki dhidi ya Lesotho Juni 10, mwaka huu Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam bila kumjumuisha mfungaji huyo wa bao la Tanzania katika sare ya 1-1 na Kenya Mei 29, mwaka 2016 kwenye mchezo wa kirafiki.
    Kikosi kitakachoingia kambini Mei 24 hadi 29 mjini Dar es Salaam kabla ya Mei 30 timu kwenda Misri kuweka kambi ya wiki moja na kurudi nchini Juni 7 kwa ajili ya mechi dhidi ya Lesotho kinaundwa na makipa; Aishi Manula (Azam), Benno Kakolanya (Yanga), Said Mohammed (Mtibwa Sugar).
    Mabeki; Shomari Kapombe, Hassan Kessy, Mwinyi Mngwali, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Salim Abdallah, Aggrey Morris (Azam), Abdi Banda (Simba) na Erasto Nyoni (Azam).  
    Viungo; Himid Mao (Azam), Jonas Mkude (Simba), Salum Abubakar ‘Sure Boy’ (Azam), Said Ndemla (Simba), Muzamil Yassin (Simba), Simon Msuva (Yanga), Farid Mussa (DC Tenerife, Hispania) na Shiza Kichuya (Simba).
    Washambuliaji ni Thomas Ulimwengu (FC Eskilstuna, Denmark), Mbwana Samatta (KRC Genk, Ubelgiji), Mbaraka Yussuf (Kagera Sugar), Ibrahim Hajib (Simba) na Abdulrahman Mussa (Ruvu Shooting).
    Ikumbukwe Mayanga anasaidiwa na Fulgence Novatus, kocha wa makipa, Patrick Mwangata, Meneja Dani Msangi, Madaktari Gilberti Kigadiya na Richard Yomba pamoja na mtunza vifaa Ally Ruvu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAGURI AMUANDIKIA ‘BARUA YA WAZI’ KOCHA MAYANGA, AMUELEZEA MAFANIKIO YAKE OMAN Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top