• HABARI MPYA

    Wednesday, May 24, 2017

    AGYEI: SIMBA HATUTARUDIA MAKOSA KWA MBAO

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    KIPA Mghana wa Simba, Daniel Agyei amesema hawatarudia makosa ya kuwaruhusu Mbao FC kuwatangulia kwa mabao katika Fainali ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) Jumamosi wiki hii Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.
    Aprili 10 mwaka huu Mbao FC iliitangulia Simba SC kwa mabao 2-0 Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara hadi dakika 10 za mwisho Wekundu wa Msimbazi walipopindua bango ghafla na kushinda 3-2.
    Daniel Agyei amesema hawatarudia makosa ya kuwaruhusu Mbao FC kuwatangulia kwa mabao katika Fainali ya ASFC Jumamosi wiki hii Uwanja wa Jamhuri, Dodoma

    Lakini kuelekea fainali ya ASFC Jumamosi, Agyei aliyesajiliwa Simba SC Desemba mwaka jana kutoka Medeama SC ya Ghana amesema hawatarudia makosa.
    “Sitarajii kama tutarudia makosa kama hayo, wote tuliona makosa tuliyoyafanya katika mchezo ule na ndiyo maana tukamalizia vizuri kwa kushinda. Safari hii tutakuwa makini sana tangu mwanzo,”amesema Agyei.
    Simba na Mbao zinakutana katika fainali ya Kombe la TFF Jumamosi Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma katika mchezo unaotarajiwa kuwa mkali na wa kusisimua.
    Hiyo inatokana na viwango vya timu zote katika mechi zao za hivi karibuni kuwa vya kuridhisha na pia matokeo ya mchezo wa mwisho baina yao Aprili 10, Mwanza.
    Simba wana kiu kubwa ya kushinda mchezo huo ili kujikatia tiketi ya kucheza Kombe la Shirikisho Afrika mwakani, baada ya kuzidiwa kete na mahasimu wao, Yanga katika Ligi Kuu.
    Lakini Mbao nao wanataka kuweka rekodi, kwanza ya kupanda na kuchukua Kombe hilo na pia kuwa timu ya pili ya Mwanza baada ya Pamba SC kucheza michuanio ya Afrika.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AGYEI: SIMBA HATUTARUDIA MAKOSA KWA MBAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top