• HABARI MPYA

    Friday, January 12, 2018

    MBEYA CITY WABADILISHA BENCHI LA UFUNDI KUELEKEA MECHI NA PRISONS JUMAPILI

    Na Mwandishi Wetu, MBEYA
    KLABU ya Mbeya City imefanya mabadiliko madogo katika benchi lake la Ufundi, ikiwaondoa kocha Msaidizi, Mohammed Kijuso na Meneja, Geoffrey Katepa.
    Mtendaji Mkuu wa MCC, Emmanuel Kimbe ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba Kijuso anakwenda kuwa Kocha Mkuu wa timu ya vijana, wakati Katepa anaondoka moja kwa moja baada ya kumaliza mkataba wake.
    Kimbe amesema kwa sasa klabu inatafuta mwalimu wa kumsaidia kocha mkuu, Mrundi Ramadhani Nswanzurino baada ya Kijuso kurejeshwa timu ya vijana, lakini hawataajiri Meneja mpya. Amesema Nswazurino kwa sasa ataendelea kusaidiwa na kocha wa makipa, Josiah Stephen katika kikosi cha kwanza.
    “Kijuso alikuwa kocha wa timu ya vijana na aliyeibua vipaji vya wachezaji kama akina Raphael Daudi ambaye amehamia Yanga. Sasa tumemrudisha kule afanye kazi nzuri ya kutuibulia vipaji vingine,”amesema Kimbe.
    Kuhusu Katepa, Kimbe amesema kwamba haikuwa sera ya Mbeya City kuajiri Mameneja, lakini walilazimika kufanya hivyo baada ya ujio wa kocha Mmalawi, Kinnah Phiri ambaye alikuwa hajui Kiswahili akahitaji mtu wa kurahisisha mawasiliano yake na wachezaji.
    “Ila baada ya Phiri kuondoka kocha aliyekuja bahati nzuri anajua Kiswahili na ndiyo maana Katepa alipomaliza mkataba wake mwezi uliopita, hatukuona sababu ya kuendelea naye,”amesema kimbe.   
    Kwa sasa Mbeya City inashika nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu kwa pointi zake 12 ilizovuna kwenye mechi 12, ikiwa inazidiwa pointi 14 na vinara Simba SC na inaizidi kwa pointi tano tu Stand united inayoshika mkia.
    MCC watateremka uwanjani Jumapili kumenyana na Tanzania Prisons Uwanja wa Sokoine katika mechi ya mahasimu wa jiji la Mbeya.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBEYA CITY WABADILISHA BENCHI LA UFUNDI KUELEKEA MECHI NA PRISONS JUMAPILI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top