• HABARI MPYA

    Tuesday, December 12, 2017

    LIPULI ‘WAIJIA JUU’ SIMBA KUHUSU ASANTE KWASI, WASEMA HAWAMUUZI MGHANA WAO

    Na Salma Suleiman, DAR ES SALAAM 
    UONGOZI wa Lipuli FC ya Iringa umekanusha kufanya mazungumzo ya aina yoyote na uongozi wa Simba SC ya Dar es Salaam kuhusu beki Mghana, Asante Kwasi.
    Tangu asubuhi kumekuwa na taarifa kwamba Lipuli imewauzia Simba beki wao huyo, Kwasi aliye katika msimu wa kwanza Uwanja wa Samora tangu asajiliwe kutoka Mbao FC ya Mwanza.
    Lakini katika taarifa yake kwa vyombo vya Habari leo, Afisa Habari wa Lipuli FC, Clement Sanga amesema kwamba hadi sasa hawajafanya mazungumzo yoyote na timu yoyote kuhusu mchezaji Asante Kwasi.
    Asante Kwasi (kushoto) akimdhibiti mshambuliaji wa Simba, John Bocco timu hizo zilipokutana Novemba 26, mwaka huu Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam na kutoa sare ya 1-1
    “Ikumbukwe mchezaji Asante Kwasi licha ya uwepo wa taarifa hizo kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii bado ni mchezaji halali wa Lipuli FC. Kwasi bado ana si chini ya miezi saba kwenye mkataba wake wa sasa na Lipuli FC na kwa muktadha huo, bado ni mchezaji halali wa Lipuli FC,”amesema Sanga.
    Kwa sasa uongozi hauna mpango wowote wa kumuuza mchezaji huyo, si kwa Simba SC tu, bali pia kwa klabu nyingine yoyote na kama hapo baadaye kutatokea ulazima wa kufanya hivyo, uongozi utatoa taarifa.
    “Tunapenda kutoa ushauri wa bure kwa timu yoyote itakayoonyesha matamanio ya kumtaka mchezaji huyo kuwasiliana na uongozi wa Lipuli FC moja kwa moja ili kuepusha misuguano isiyokuwa na ulazima kwa afya ya familia ya mchezo wa soka nchini,”amesema Sanga.
    Kwasi aliikatili Simba kubeba pointi tatu mbele ya Lipuli Novemba 26, mwaka huu baada ya kufunga bao la kusawazisha katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara timu hizo zikitoka sare ya 1-1 Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: LIPULI ‘WAIJIA JUU’ SIMBA KUHUSU ASANTE KWASI, WASEMA HAWAMUUZI MGHANA WAO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top