• HABARI MPYA

    Monday, June 29, 2015

    STEVE NYERERE ATANGAZA NIA YA KUGOMBEA UBUNGE KINONDONI

    Na Asha Said, DAR ES SALAAM
    MSANII wa filamu nchini Steven Mengere 'Steve Nyerere' (pichani) amewataka watanzania wenzake kujitokeza kuandikisha katika daftari la wapiga, ili wasikose kupiga kura katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi Oktoba mwaka huu.
    Akizungumza katika mkutano maalum wa kutangaza nia na kuhamasisha watu kujiandikisha, alisema kujiandikisha ni haki ya kila Mtanzania hivyo kwa vijana na wazee hakuna sababu ya kukaa na kuacha muda unapioga bila ya kuutumia.
    Nyerere alisema ni haki kwa kila Mtanzania kwenda kujiandikisha hivyo hakuna sababu ya kuacha kipindi hicho kinapita bila ya wao kukitumia.

    Msanii Steven Mengele 'Steve Nyerere' akiwasili katika viwanja vya CCM Bwawani, kuongea na wananchi wa eneo hilo, kwa ajili ya kutangaza nia ya kugombea Ubunge wa jimbo la Kinondoni, ikiwa pamoja na kuhamasisha wananchi wajitokeze kujiandikisha. Msanii wa filamu Tanzania Steven Mengele 'Steve Nyerere' na mkewe wakisalimia na wananchi waliojitokeza katika mkutano wake wa kutangaza kuwania jimbo la Kinondoni.‏

    "Mama zangu, Baba zangu, Vijana wenzangu, jitokezeni kujiandikisha ni haki yenu ya msingi, hasa katika uchaguzi mkuu ujao"alisema Steve Nyerere.
    Pia Nyerere alisema atahakikisha anatatua changamoto za wananchi wa jimbo la Kinondoni pindi atakapopata ridhaa ya kuliongoza jimbo hilo.
    Hayo aliyasema juzi wakati akitangaza nia ya kuwania ubunge wa Kinondoni kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
    Msanii huyo alisema wilaya hiyo ina changamoto nyingi ambazo zinapaswa kutatuliwa ili wananchi waweze kuishi maisha ambayo hayana kero.
    Alisema huu ni wakati wa mabadiliko na mabadiliko yataletwa na yeye kwa kuwa anazijua changamoto nyingi ambazo zinawakabili wananchi hao.
    "Mimi Steve Nyerere nimeamua kwa dhati kujitoa na kutangaza nia ya kuwania ubunge ili nisaidiane na wananchi wa Kinondoni kwa ajili ya kuijenga Kinondoni mpya," alisema Steve.
    Alisema Kinondoni inapaswa kuwa ya mfano kwa kuwa na mitaa iliyopangwa katika mpangilio maalumu na mitaro iliyosafishwa vyema.
    Alisema licha ya hilo, Kinondoni inapaswa kuboreshwa miundombinu ili kuzuia mafuriko ambayo yamekuwa yakitokea mara kwa mara na kuharibu sifa ya jimbo hilo linaloubeba mkoa wa Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: STEVE NYERERE ATANGAZA NIA YA KUGOMBEA UBUNGE KINONDONI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top