• HABARI MPYA

    Saturday, November 16, 2013

    HUMOUD ATIMULIWA ZANZIBAR HEROES, KOCHA ZANZIBAR ADHALILISHA MWANDISHI WA HABARI

    Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
    KIUNGO wa timu ya Taifa ya Zanzibar ‘The Zanzibar Heroes’ Abdulhalim Humoud, ametimuliwa katika kikosi hicho baada ya kushindwa kuripoti kambini na wenzake.
    Taarifa zilizopatikana na mwandishi wa habari hizi jana, zimefahamisha kuwa, mchezaji huyo aliyesajiliwa na Simba SC ya Dar es Salaam, ambaye alikuwa Zanzibar akifanya mazoezi na timu hiyo, wakati timu ikiingia kambini hoteli ya Bwawani Jumatatu wiki hii jioni, hakutokea.
    Abdulhalim Humud amefungiwa vioo Zanzibar Hereos 

    Kocha msaidizi wa Zanzibar Heroes Saleh Ahmed ‘Machupa’, amesema kitendo cha Humoud kutokuripoti kambini bila ya taarifa, kinahesabiwa kuwa ni utovu wa nidhamu ambao kocha mkuu Salum Bausi amesema hawezi kukivumilia.  
    Hata hivyo, Ahmed alisema siku ya pili yaani Jumanne ya Novemba 11 nyakati za jioni, mmoja kati ya ndugu wa mchezaji huyo alikwenda Bwawani iliko kambi ya Zanzibar Heroes, na kusema kuwa kiungo huyo amesafiri kwenda Dar es Salaam kutokana na matatizo ya kifamilia.
    “Yawezekana kama kweli Humud ana matatizo lakini wakati alikuwepo hapa angeweza kuja kambini na kutufahamisha badala ya kuondoka na baadae kutuma mtu. Huo si utaratibu,” alisema Machupa, baba wa mchezaji Adeyoum Saleh ambaye pia yumo katika kikosi hicho.
    Alieleza kuwa, kukosekana kwa mchezaji huyo hakutaiathiri timu hiyo, kwani jana, wachezaji watatu walikuwa katika timu ya Taifa ya Tanzania, Khamis Mcha ‘Viali’, Waziri Salum na mlinda mlango Mwadini Ali, walitarajiwa kuwasili kambini baada ya kuachwa katika kikosi cha Stars kitakachoivaa Harambee Stars ya Kenya katika mechi ya kirafiki Jumanne ijayo.
    Wakati huohuo, mwandishi wa habari wa kituo cha televisheni cha Chanel Ten anayefanyia kazi hapa Zanzibar Munir Zakaria, ametishia kumpandisha mahakamani kocha mkuu wa Zanzibar Heroes Salum Bausi iwapo hatamuomba radhi kwa madai kuwa kocha huyo amemdhalilisha kwa kummwagia matusi ya nguoni hadharani.
    Zakaria alikumbwa na kadhia hiyo jana asubuhi, wakati alipokwenda uwanja wa Mao Tse Tung kufuatia mazoezi ya Zanzibar Heroes kwa ajili ya kuripoti kwenye kituo chake anachofanyia kazi, ambapo kocha Bausi aliamua kumshambulia kwa maneno, akionesha kukerwa na suala la mwandishi huo alilomuuliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Ikulu Jumanne iliyopita.  
    Katika mkutano wa Mheshimiwa Rais na waandishi wa habari, Zakaria alidai kuwa, Rais ndiye aliyeiambia ZFA imrejeshe Bausi kuifundisha timu hiyo, wakati wananchi na baadhi ya wachezaji hawamtaki, jambo ambalo Rais alikanusha na kutoa ufafanuzi juu ya alichosema siku alipotembelewa na ujumbe wa Wazee SC akiwemo Rais wa ZFA Ravia Idarous. 
    Kufuatia mashambulizi hayo ya maneno na kutimuliwa uwanjani hapo, Zakaria amemwambia mwandishi wa habari hizi aliyeshuhudia kadhia hiyo, kuwa anampa Bausi siku saba kuomba radhi, vyenginevyo atampandisha kizimbani kudai fidia ya kuvunjiwa heshima kadamnasi, na kwamba anaendelea kujadiliana na mwanasheria wake.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: HUMOUD ATIMULIWA ZANZIBAR HEROES, KOCHA ZANZIBAR ADHALILISHA MWANDISHI WA HABARI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top