• HABARI MPYA

    Wednesday, November 27, 2013

    CECAFA CHALLENGE 2013; ACHA MOTO UWAKE NAIROBI

    Na Mahmoud Zubeiry, Nairobi
    KOMBE la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Challenge, michuano yake ya mwaka huu inaanza leo mjini hapa, timu zote 12 zinazotarajiwa kushiriki zikiwa tayari kituoni. Pata wasifu wa timu hizo na ratiba.
    NYOTA WA HARAMBEE:
    Kenya ambayo timu yake ya taifa inaitwa Harambee Stars, imeshiriki mara tano fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, ingawa haijawahi kuingia raundi ya pili zaidi ya kunusa na kutolewa. Ilishiriki michuano ya kuwania kucheza fainali za Kombe la Dunia kwa mara yakwanza mwaka 1974 na imeendelea hadi fainali za mwaka huu zilizofanyika Afrika Kusini, lakini haijafanikiwa kufuzu.
    Mwaka 2004, FIFA iliisimamisha Kenya kushiriki michuano yote ya kimataifa kwamiezi mitatu, kufuatia serikali ya nchi hiyo kuingiliwa masuala ya soka, lakini kifungo hicho kilisitishwa baada ya nchi hiyo kukubalia kufuata masharti ya shirikisho hilo la kimataifa la soka.
    Oktoba 25, mwaka 2006, Kenya ilisimamishwa tena katika soka ya kimataifa kwa kushindwa kutekeleza makubaoliano yaliyofikiwa Januari mwaka huo ya kutatua matatizo yaliyokuwa yametawala kwenye shirikisho lao la soka, hata hivyo walipomaliza matatizo yao adhabu yao ilifutwa. Kenya waliosyhiriki fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mara nne, katika miaka ya 1988, 1990, 1992 na 2004 na mara zote wakitolewa raundi ya kwanza, ni mabingwa mara tano wa Kombe la Challenge la CECAFA katika miaka ya 1975, 1981, 1982, 1983 na 2002, wakati pia imeshika nafasi ya pili mara tano.

    MWEWE WA JANGWANI;
    TIMU ya taifa ya Sudan inajulikana kwa jina la utani kama Sokoor Al-Jediane Kiarabu, Kiingereza Desert Hawks, yaani Mwewe wa Jangwani.
    Hii ilikuwa moja ya nchi tatu tu nyingine zikiwa ni Misri na Ethiopia zilizoasisi Kombe la Mataifa Huru ya Afrika mwaka 1957 na ilifanikiwa kushinda taji hilo mwaka 1970, wakiwa wenyeji, baada ya kuwafunga Ghana 1-0 kwenye fainali, wakitoka kuifunga Misri 2-1 katika Nusu Fainali. Sudan ni miongoni mwa timu kongwe barani Afrika na ilikuwa ina historia ya utajiri miaka ya 1950 na 1970.
    Sudan pia ilishika nafasi ya pili kwenye michuano hiyo katika fainali za mwaka 1959 zilizofanyika mjini Cairo, Misri zikishirikisha nchi tatu, yani mbali na wenyeji, pia walikuwapo Ethiopia. Ilishika tena nafasi ya pili katika fainali za mwaka 1963 baada ya kufungwa na Ghana 3-0 kwenye fainali, wakati 1957 ilikuwa ya tatu. Sudan pia wametwaa mara tatu Kombe la Challenge katika miaka ya 1980, 2006 na 2007 na wamekuwa wa pili mara mbili 1990 na 1996 na washindi wa tatu mara mbili pia, 1996 na 2004.

    KORONGO WA KAMPALA; 
    Uganda ambayo timu yake ya taifa inaitwa The Cranes, yaani Korongo hawajawahi kufuzu kwenye fainali za Kombe la Dunia, na kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika matokeo yao mazuri kabisa ni kushika nafasi ya pili mwaka 1978, baada ya kufungwa na wenyeji Ghana 2-0 mjini Accra.
    Lakini Korongo wa Uganda wanajivunia kuwa timu iliyotwaa mara nyingi zaidi taji (mara 13) la Challenge, katika miaka ya 1973, 1976, 1977, 1989, 1990, 1992, 1996, 2000, 2003, 2008 na 2009, 20111 na 2012 na pia imeshika nafasi ya pili mara nne.

    NYIGU WA KIGALI;
    Rwanda ambayo timu yake ya taifa inaitwa Amavubi Kinyarwanda, yaani  (The Wasps),  yaani Nyigu, pamoja na kwamba walichelewa kuingia kwenye soka ya kimataifa kutoka muda mrefu wa kutokuwa na amani nchini mwao, lakini tangu wamefunguliwa milango wanaonekana kuwa tishio. Walikuwapo kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2004 nchini Tunisia na wana taji moja la Challenge walilotwaa mwaka 1998, wakati wamekwishakuwa washindi wa pili mara tano katika miaka ya 2003, 2005, 2007, 2009 na 2010 na wameshika nafasi ya tatu mara tatu katika miaka ya  2001, 2002 na 2006.

    MBAYUWAYU WA BUJUMBURA;
    Burundi ambayo timu yake ya taifa inaitwa Int’hamba Murugamba Kirundi, Les Hirondelles Kifaransa au The Swallows Kiingereza yaani Kiswahili Mbayuwayu, hii kwa pamoja na Eritrea na Djibouti ndio zinaweza kuwa zenye mafanikio duni kabisa katika ukanda wa CECAFA, kwani hazijawahi kushinda hata taji moja la Challenge wala hata kunusa kwenye fainali za Matafa ya Afrika.
    Lakini ni nchi ambayo imebarikiwa wachezaji wenye vipaji, ingawa wengi baadaye huikana nch hiyona kuchukua uraia wan chi jirani, kwa mfano Nonda Shabani aliyehamia DRC na Hamadi Ndikumana aliyajivika Unyarwanda. Lakini katika kizazi cha sasa inao wakali kama Suleiman Ndikumana, anayecheza Ubelgiji. 

    RISASI ZA SHABA;
    Zambia iliyokuwa ikijulikana kama Rhodesia ya Kaskazini zamani, timu yake ya taifa inaitwa Copper bullets au Chipolopolo kama wajiitavyo wenyewe; yaani risasi za shaba, imefika mara mbili katika fainali kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika, kwanza 1974 ikafungwa 2-0 na Zaire na mara ya pili 1994, ikafungwa 2-1 na Nigeria. Fainali nyingine za Kombe hilo ilizoshiriki ni za 1978 (Raundi ya kwanza), 1982 (Nafasi ya tatu), 1986 (Raundi ya kwanza), 1990 (Nafasi wa tatu), 1992 (Robo Fainali), 1996 (Nafasi ya tatu), 1998 (Raundi ya kwanza), 2000 (Raundi ya kwanza), 2002 (Raundi ya kwanza), 2006 (Raundi ya kwanza), 2008 (Raundi ya kwanza) na 2010 (Robo Fainali).
    Lakini pia inajivunia kuifunga 4-0 Italia katika michuano ya Olimpiki mwaka 1988 mjini Seoul, Korea Kusini, siku ambayo Kalusha Bwalya alifunga mabao matatu peke yake.
    Ina mataji matatu ya Kombe la COSAFA iliyotwaa katika miaka ya 1997, 1998 na 2006, imekuwa ya pili mara tatu pia katika miaka ya 2004, 2005 na 2007, wakati kabla ya kuhamia kusini mwa Afrika ilipokuwa CECAFA, ilitwaa taji hilo mara mbili katika miaka ya 1984 na 1991 na kushika nafasi ya pili mara nne katika miaka ya 1976, 1977, 1978 na 1988. Baada ya kuhamia COSAFA, katika kualikwa kwake CECAFA, ilitwaa taji hilo mwaka 2006, lakini haikuruhusiwa kuondoka nalo, wakakabidhiwa waliokuwa washindi wa pili Sudan.

    MABAHARIA WA MOGADISHU;
    Somalia ambayo timu yake ya taifa inafahamika kama The Ocean Stars, yaani Nyota wa Bahari ni nchi mwanachama wa mashirikisho ya mawili ya soka; kwanza Afrika (CAF) na pili Urabuni (UAFA). Haijawahi kufuzu kwenye fainali za Kombe la DUnia wala Mataifa ya Afrika na kwa sasa imezuiwa kucheza mechi nyumbani kwake, Somalia kutokana na vita ya wenyewe kwa wenyewe inayoendelea. Mechi zake zote za kuwania tiketi ya kucheza fainali za Mataifa ya Afrika, inachezea ugenini.

    MASHUJAA WA VISIWANI;
    Zanzibar ambayo timu yake ya taifa inajulikana kama Zanzibar Heroes, au Mashujaa wa Visiwa vya Karafuu, kwenye soka ya kimataifa bado ni sehemu ya Tanzania, ingawa inapigania uanachama wake FIFA, ili iwe taifa kamili katika dunia ya soka. Lakini kwa CECAFA, Zanzibar inaingia kama nchi na imewahi kutwaa ubingwa wa michuano hiyo mwaka 1995, ikiwafunga wenyeji Uganda 1-0.
    Zanzibar pia imewahi kuinmgia Nusu Fainali mara sita na mara tatu ikishika nafasi ya tatu, wakati michuano ya mwaka huu, inaeonekana kuwa na kikosi imara zaidi. 

    SWALA DUME;
    Ethiopia ambayo timu yake ya taifa inajulikana kama The Walya Antelopes, mchanganyiko wa maneno mawili, la Kiingereza na Kihabeshi, lenye maana ya ‘Swala dume’ ni miongoni mwa nchi tatu pamoja na Misri na Sudan zilizoasisi michuano ya Mataifa Huru ya Afrika mwaka 1957 na wakafanikiwa kutwaa taji hilo mwaka 1962 walipokuwa wenyeji, ingawa baada ya muongo huo, imepoteza makali yake. Inajivunia kutwaa mataji ya Challenge katika miaka ya 1987, 2001, 2004 na 2005.

    NYOTA WA KILIMANJARO;
    Tanzania, ambayo kabla ilikuwa ikijulikana kama Tanganyika, timu yake ya taifa inaitwa Kilimanjaro Stars- ingawa nje ya michuano ya CECAFA inatambulika kama Taifa Stars, kwa sababu inaungana na Zanzibar kuunda timu moja.
    Haijawahi kushiriki fainali hata moja za Kombe la Dunia, lakini inajivunia kucheza fainali moja za mwaka 1980 za Kombe la Mataifa ya Afrika nchini Nigeria, sambamba na kutwaa mara tatu Kombe la Challenge katika miaka ya 1974, 1994 na 2010 na kushika nafasi ya pili mara tano. 

    SUDAN KUSINI, TAIFA JIPYA
    Huyu ni mwanachama mpya wa CECAFA, Sudan Kusini ambayo imejitenga kutoka Sudan. Sudan Kusini ilishiriki michuano ya kwanza ya Challenge mwaka 2012 mjini Kampala, Uganda walipopangwa pamoja na Ethiopia, Kenya na wenyeji Uganda katika Kunsi A. Walifungwa mechi zote, na Ethiopia 1-0 bao pekee la Yonathan Kebede, 2-0 na Kenya na 4-0 na Uganda, Brian Umony akifunga mawili, mengine Robert Ssentongo na Hamis Kizza. Je, wamekuja na jipya gani katika Challenge ya mwaka huu?  Tutaona.

    WAZAMIAJI WA ERITREA
    Tayari imeingia katika orodha ya wanachama wa muda mrefu wa CECAFA, lakini haina mafanikio yoyote katika mashindano hayo na wala haijawahi hata kunusa Kombe la Mataifa ya Afrika wala Kombe la Dunia. Miaka ya karibuni wachezaji wa Eritrea walikuwa wanazamia nchi za watu wakienda kwenye mashindano mbalimbali, hali ambayo ilifanya isimamishwe na CECAFA kucheza mashindano hayo hadi hapo itakapoona inaweza kudhibiti wachezaji wake kuzamia nchi za watu na kwa kurejea mwaka huu, maana yake tayari wamepata ufumbuzi wa tatizo hilo.

    RATIBA HATUA YA MAKUNDI;
    Wed. 27th Nov. 2013
    Zanzibar Vs S. Sudan A NYAYO 2.00PM
    Kenya - Vs Ethiopia A NYAYO 4.30PM
    Thur. 28th Nov. 2013
    Burundi VS Somalia B MACHAKOS 2.00PM
    Tanzania VS  Zambia B MACHAKOS 4.00PM
    Fri. 29th Nov. 2013
    Sudan Vs Eritrea C MACHAKOS 2.00PM
    Uganda Vs Rwanda C MACHAKOS 4.00PM
    Sat.30th Nov. 2013
    Ethiopia Vs Zanzibar A NYAYO 2.00PM
    S.Sudan  Vs Kenya A NYAYO 4.00PM
     Sun. 1st. Dec. 2013
    Somalia Vs Tanzania B NYAYO 2.00PM
    Zambia  Vs Burundi   B NYAYO 4.00PM
    Mon. 2nd   Dec. 2013
    Sudan  Vs Rwanda C MACHAKOS 2.00PM
    Eritrea  Vs Uganda C MACHAKOS 4.00PM
    Tue. 3rd  Dec. 2013
    S.Sudan  Vs Ethiopia A MACHAKOS 2.00 PM
    Kenya  Vs Zanzibar A MACHAKOS 4.00PM
    Wed. 4th    Dec. 2013
    Tanzania Vs   Burundi B NYAYO 2.OOPM
    Somalia   Vs Zambia B NYAYO 4.00PM
    Rwanda VS   Eritrea C NYAYO 2.00PM

    Uganda VS    Sudan C NYAYO 400PM
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: CECAFA CHALLENGE 2013; ACHA MOTO UWAKE NAIROBI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top