• HABARI MPYA

    Friday, November 22, 2013

    MCHEZAJI ATIMULIWA ZANZIBAR HEROES KWA 'KUCHAPA DEMU’ USIKU KUCHA

    Na Mwandishi Wetu, Zanzibar 
    KASHFA ya ngono imeibuka ndani ya kambi ya  timu ya Taifa ya Zanzibar Heroes iliyoko hoteli ya Bwawani, ambapo mchezaji mmoja (jina linahifadhiwa), ametimuliwa kwa kitendo cha kupenyeza mwanamke kambini.
    Hayo yanajiri zikiwa zimebaki siku tatu tu kabla kikosi cha timu hiyo kufunga safari ya Kenya kushiriki michuano ya Chalenji inayotarajiwa kuanza Novemba 27, ambapo Zanzibar itashuka dimbani siku hiyo kuivaa Sudan Kusini katika mechi ya kwanza ya kundi A. 
    Nidhamu kwanza; Kocha wa Zanzibar Heroes amekuwa mwenye msimamo mkali dhidi ya wachezaji watovu wa nidhamu

    Ingawa hatua hiyo imefanywa kimyakimya, uchunguzi wa Zanzibar Leo umegundua kuwa, mchezaji huyo amekiuka taratibu na nidhamu ya kambi, ambapo takriban siku tatu amekuwa akiingiza mwanamke na kulala naye hadi majogoo, na kumtoa alfajiri.
    Chanzo cha uhakika kimeliambia gazeti hili kuwa, baada ya kubaini hali hiyo, baadhi ya wafanyakazi wa hoteli hiyo waliokuwa karibu na timu, walijaribu kumuasa mchezaji huyo aache tabia hiyo, wakimuambia kuwa inaweza kumuharibia.
    Hata hivyo, licha ya kupewa ushauri huo wa bure, mchezaji huyo anayechezea Mtibwa Sugar ya Morogoro katika ligi kuu Tanzania Bara, alitia pamba masikioni na kupuuza nasaha za wasamaria wema hao.      
    Baada ya kuchoshwa na tabia hiyo, baadhi ya wasamaria waliamua kuupasha uongozi wa timu hiyo, ambapo nao ulimuita mchezaji huyo na kumwaga taarifa hizo.
    Taarifa zilizopatikana na gazeti hili kutoka ndani ya kambi ya timu hiyo, zilifahamisha kuwa mwanandinga huyo alishindwa kujitetea wakati alipomwagiwa kashfa yake, hali iliyoufanya uongozi kutokuwa na shaka juu ya madai ya utovu huo wa nidhamu.
    Hatua ya kumfukuza mchezaji huyo imefanyika juzi, ambapo baada ya kusomewa ‘gazeti’ lake na kushindwa kukanusha, aliamriwa kufungasha virago na kuondoka kambini mara moja.
    Huyo anakuwa mchezaji wa pili kufurushwa Zanzibar Heroes, baada ya kiungo wa Simba Abdulhalim Humoud kutimuliwa wiki moja iliyopita kwa kuondoka kambini bila taarifa kwa madai ya kutingwa na matatizo ya kifamilia jijini Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MCHEZAJI ATIMULIWA ZANZIBAR HEROES KWA 'KUCHAPA DEMU’ USIKU KUCHA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top