• HABARI MPYA

    Friday, November 29, 2013

    AZAM YAVULIWA UBINGWA KOMBE LA UHAI, YANGA KUTINGA FAINALI LEO?

    Na Prince Akbar, Dar es Salaam
    COASTAL Union ya Tanga, jana imetinga Fainali za michuano ya vijana chini ya umri wa miaka 20 kwa klabu za Ligi Kuu ya Bara, maarufu kama Kombe la Uhai, baada ya kuwafunga waliokuwa mabingwa watetezi, Azam FC bao 1-0, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi.
    Bao pekee la Wagosi wa Kaya jana lilifungwa na mshambuliaji Yussuf Chipo dakika ya 32 na sasa timu hiyo ya Tanga inasubiri mshindi kati ya Yanga SC, na Mtibwa Sugar mechi inayochezwa leo Uwanja wa Azam.
    Abdallah Mguhi 'Messi' ataiongoza Yanga SC katika mchezo na Mtibwa Sugar leo

    Yanga ilitinga Nusu Fainali juzi baada ya kuichapa Ashanti United kwa mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa  kwenye Uwanja wa Azam Complex pia, .
    Bao la ushindi kwa Yanga lilipachikwa wavuni na winga Abdallah Mguhi ‘Messi’ dakika ya 84 ya mchezo huo baada ya kuwazidi ujana walinzi wa Ashanti United.
    Yanga iliwachukua dakika 21 kupata bao la uongozi lililofungwa na Hamis Issa wakati Ashanti walisawazisha kupitia Ally Kabunda  dakika ya 62 kwa mkwaju wa penalti.
    Kabunda ambaye ni mtoto wa beki wa zamani wa Yanga, Salum Kabunda ‘Ninja’ anawania tuzo ya mfungaji bora baada ya kufunga mabao tisa huku Ibrahim Hajibu wa Simba na Patrick Madidi wa Mtibwa Sugar wakiwa na mabao manne kila mmoja.
    Fainali inatarajiwa kuchezwa Jumapili wiki hii Uwanja wa Azam Complex.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM YAVULIWA UBINGWA KOMBE LA UHAI, YANGA KUTINGA FAINALI LEO? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top