• HABARI MPYA

    Sunday, January 14, 2018

    SIMBA YALETA KOCHA MFARANSA ALIYEFUNDISHA MAZEMBE, ETOILE DU SAHEL, SETIF NA USM ALGER

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KOCHA wa zamani wa klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Etoile du Sahel ya Tunisia, Mfaransa, Hubert Velud amewasili mjini Dar es Salaam leo kukamilisha mipango ya kujiunga na klabu ya Simba.
    Habari kutoka ndani ya Simba zimesema kwamba, Velud mwenye umri wa miaka 58 analetwa na mmiliki mtarajiwa wa klabu hiyo, Mohamed ‘Mo’ Dewji. 
    Velud pia alikuwa kocha wa timu ya taifa ya Togo na alipigwa risasi mkononi wakati basi la wachezaji liliposhambuiliwa na waasi Angola wakati wanakwenda kwenye fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2010.
    Mfaransa, Hubert Velud amewasili mjini Dar es Salaam leo kukamilisha mipango ya kujiunga na klabu ya Simba

    Ana uzoefu wa kufundisha timu nyingi kama Chalons-sur-Marne, Gap, Paris FC, Gazelec Ajaccio, Clermont, Cherbourg, Creteil, Toulon na Beauvais.
    Ameshinda katika Ligue 1 ya Algeria mwaka 2013 akiwa ES Setif, 2014 akiwa na USM Alger na Super Cup ya Algeria mwaka 2013 akiwa na USM Alger.
    Anakuja Simba kuchukua nafasi ya Mcameroon, Joseph Marius Omog aliyefukuzwa Desemba baada ya msimu mzuri akiiwezesha timu hiyo kurudi kwenye michuano ya Afrika baada ya miaka minne.
    Velud aliyezaliwa Juni 8, mwaka 1959 mjini Villefranche-sur-Saône, Ufaransa enzi zake alikuwa kipa mzuri na alidakia timu za Reims kati ya 1976 na 1989 na Chalons-sur-Marne kati ya 1989 na 1990 kabla ya kuwa kocha.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YALETA KOCHA MFARANSA ALIYEFUNDISHA MAZEMBE, ETOILE DU SAHEL, SETIF NA USM ALGER Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top