• HABARI MPYA

    Monday, December 04, 2017

    KAMUSOKO KUANZA KUCHEZA TENA YANGA MWAKA MPYA, 2018

    Na Salma Suleiman, DAR ES SALAAM
    KIUNGO Mzimbabwe wa Yanga, Thabani Scara Kamusoko anaweza kuanza tena kucheza mapema Januari, 2018 iwapo matibabu anayoendelea kupatiwa na Umoja wa Madaktari wenye mapenzi na klabu yake kutoka hospitali ya Temeke, Dar es Salaam yatafanikiwa.
    Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Chama cha Madaktari wa Michezo Tanzania (TASMA), Dk. Nassor Matuzya katika mahojiano maalum na Bin Zubeiry Sports – Online leo mjini Dar es Salaam.
    Dk. Matuzya amesema baada ya vipimo alivyofanyiwa wamegundua ana tatizo la ndani ya goti lake la mguu wa kushoto ambalo baada ya matibabu yatakayokamilika wiki hii, atahitaji mapumziko ya wiki mbili kabla ya kuanza mazoezi mepesi.
    Thabani Kamusoko anaweza kuanza tena kucheza mapema Januari kama matibabu haya yatafanikiwa 
    Dk. Nassor Matuzya (kushoto) na mwenzake (kulia) wakimpatia matibabu Thabani Kamusoko 

    “Ni matumaini yangu kama zoezi hili tunaloendelea nalo litafanikiwa, basi Kamusoko aterejea uwanjani Januari akiwa mwenye nguvu zaidi na tatizo hili halitamsumbua tena,”amesema Dk. Matuzya ambaye ameunda jopo maalum la madaktari wenye mapenzi na Yanga katika hospitali ya Temeke kumtibu mchezaji huyo.
    Na Matuzya, Daktari wa zamani wa Yanga, aliunda jopo hilo baada ya kuguswa na maumivu ya mchezaji huyo ambaye yuko nje kwa muda mrefu na kushindwa kuisaidia klabu yake.  
    “Kamusoko alikuwa anataka msaada wa daktari anayeweza kumsaidia. Tangu mwanzo mimi ndiye niliyejua ana tatizo gani, lakini niliamini angeweza kutibiwa na klabu. Lakini alipoona siku zinaenda na hapati ahueni yoyote, akaja kwangu,”amesema Matuzya ambaye kwa sasa yupo hospitali ya Temeke.
    Matuzya amesema kwamba akaamua kuwashirikisha Madaktari wenzake wa vitengo tofauti na fani tofauti katika hospitali ya Temeke, ambao ni wapenzi wa Yanga pia – ndipo akaunda jopo hilo.
    “Tulimfanyia uchunguzi wa kina, tukianza tukianza na vipimo vya mionzi (X-ray na MRI) na baada ya kugundua tatizo,tukaanza kjmtibu ingawa tumshukuru mdau mmoja wa Yanga aliyetusaidia fedha za gharama za matibabu,”amesema Matuzya.

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KAMUSOKO KUANZA KUCHEZA TENA YANGA MWAKA MPYA, 2018 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top