• HABARI MPYA

    Wednesday, February 13, 2019

    MTIBWA SUGAR YAHAMISHIA HASIRA ZAKE KWA BIASHARA UNITED KESHO

    Na Mwandishi Wetu, MOROGORO
    BAADA ya kipigo cha 1-0 kutoka kwa Mwadui FC mapema wiki hii kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Mtibwa Sugar imehamishia hasira zake kwenye mchezo ujao dhidi ya Biashara United ya Mara kesho.
    Jumatatu wiki hii, Mwadui FC iliilaza Mtibwa Sugar 1-0, bao pekee la mshambuliaji wake tegemeo, Salim Ayeye dakika ya 75 Uwanja wa Mwadui Comoplex mjini Shinyanga.
    Matokeo hayo yanaifanya Mtibwa SUgar ibaki na pointi 29 baada ya kucheza michezo 22 na kushikilia nafasi ya 11 katika msimamo wa ligi kuu bara (Tanzania Premier League).
    Lakini kuelekea mchezo ujao wa Ligi Kuu dhidi ya Biashara, Msemaji wa Mtibwa Sugar  Thobias Kifaru Ligalambwike amesema watarejesha heshima.
    Mtibwa Sugar imehamishia hasira zake kwenye mchezo ujao dhidi ya Biashara United ya Mara kesho

    “Tumetoka kupoteza sio jambo zuri kwetu, lakini niwaombe wapenzi wa Mtibwa kuwa na amani hali itatengamaa na tunashinda mchezo ujao dhidi ya Biashara siku Alhamisi nimeomgea na benchi la ufundi chini ya Zuber Katwila wamenihakikishia kufanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza katika michezo iliyopita, kwa kudra za mwenyezi  Mungu tunataraji kuingia Mara jioni ya leo" amesema Kifaru.
    Kifaru alisema moja ya sababu za Mtibwa Sugar kufanya vibaya katika michezo ya karibuni ni kukosa baadhi ya nyota wake muhimu.
    “Tumefanya vibaya katika michezo ya karibuni na hii inatokana na kukosa baadhi ya wachezaji wetu muhimu tumemkosa Hassan Isihaka ambaye anaumwa malaria, Kibwana Shomari yeye ana majeraha ya goti, Ismail Mhesa 'Chomeka' anaumwa enka, Saleh Khamis anasumbuliwa na maumivu ya mguu sehemu ya nyuma ya kisigino, Salum Kihimbwa anaumwa malaria,  Dickson Daud amefiwa na mama mkwe wake ameenda kuhudhulia msiba," 
    "Dickson Job na Kelvin Sabato  walikuwa wameenda katika majaribio na tayari wamerejea lakini hawatajumuishwa katika mchezo ujao, Issa Rashid “Baba Ubaya” alikosa mchezo uliopita dhidi ya Mwadui kwasababu alikuwa anatumikia adhabu ya kadi tatu za njano," amesema Kifaru.
    Wachezaji ambao wako safarini  kwa ajili ya mchezo wa Biashara kesho ni Makipa Shaaban Hassan Shaaban “Kado”, Abuutwalib  Hamidu Mshery , Benedict Tinocco Mlekwa na kwa upande wa Mabeki ni  Salum Kanoni Kupela “Mbavu Kunesa”, Cassian Ponera Cassian, Nickson Clement Kibabage, Ally Shomary Shareef, Issa Rashid Issa “Baba Ubaya” na Hussein Idd Abdallah.
    Viungo  walio safiri kuelekea Musoma kuwafuata Biashara ni  Awadh Juma “Maniche”, Ayoub Semtawa, Haruna Chanongo, Ally Yusuf Makarani, Henry Joseph Shindika, Shaaban Mussa Nditi na Nassor Seif Kiziwa na katika nafasi ya ushambuliaji  waliosafiri ni Juma Ally Luizio, Abdul Yusuf Haule, Riphat Khamis Msuya na Jaffari Salum Kibaya.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MTIBWA SUGAR YAHAMISHIA HASIRA ZAKE KWA BIASHARA UNITED KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top